UN, IOM zalaani mauaji ya wakimbizi 42 wa Kisomali, pwani ya Yemen.

Shirika la Kimataifa la Wahajiri (IOM) limekosoa vikali shambulio lililoua makumi ya wakimbizi raia wa Somalia katika pwani ya Yemen usiku wa kuamkia jana.

Mohammed Abdikheir, Mkurugenzi wa Masuala ya Dharura wa IOM amesema kuwa, shambulio hilo dhidi ya boti ya wakimbizi karibu na Lango Bahari la Bab al-Mandab katika mkoa wa Hodeida, pwani ya Yemen halikubaliki. 


Amesema waliotekeleza shambulio hilo wangestahili kuangalia kwa makini waliokuwa kwenye boti hiyo kabla ya kuchukua hatua yoyote.

Inaarifiwa kuwa, boti hiyo ilikuwa inatoka Yemen kuelekea Sudan wakati iliposhambuliwa kwa kombora kutoka angani saa tisa usiku, kuamkia Ijumaa ya jana.

Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) pia limelaani mauaji hayo ya wakimbizi na kuandika katika katika ukurasa wake rasmi wa mtandao wa kijamii wa Twitter kuwa: 

Tumeshangazwa na shambulio hili, ni hujuma ya hivi punde dhidi raia wasio na hatia, na mwendelezo wa matokeo hasi ya mgogoro wa Yemen. La kusikitisha zaidi ni kuwa, wakimbizi hao ni halali ambao tunawatambua na wana vyeti halali vya shirika hili."

Harakati ya Ansarullah ya Yemen imetangaza kuwa muungano wa kijeshi wa Saudi Arabia ndio uliohusika na hujuma hiyo ya kikatili ya wakimbizi ambao walikuwa hawajajizatiti kwa silaha.
Wakimbizi wa Kisomalia zaidi ya 42 wameuawa katika hujuma hiyo huku makumi ya wengine wakijeruhiwa.
 chanzo;parstoday.

Comments