Hata hivyo, shirika hilo limesisitiza kuwa wale wote watakaokaidi
kulipa madeni yao, litaendelea na utaratibu wake kuwakatia huduma ya
umeme kama lilivyoahidi.
Hayo yalibainishwa Dar es Salaam na Kaimu Meneja Uhusiano wa shirika
hilo, Leila Muhaji wakati alipozungumza na gazeti hili kwa njia ya simu
kuhusu mwitikio wa wadaiwa wa Tanesco baada ya siku 14 zilizotolewa na
shirika hilo kumalizika.
“Kwa sasa tunachofanya ni kukusanya taarifa kutoka kwa mameneja wa
mikoa waliopewa kazi ya kusimamia utaratibu huo wa wanaolipa madeni
yao,” alisema Muhaji na kufafanua kuwa, menejimenti ya shirika hilo
imejipanga kuhakikisha kuwa wale wote ambao hawatatimiza wajibu wao na
kulipa madeni yao, kukatiwa huduma za umeme.
“Pia tutatoa taarifa kuhusu mwitikio wa waliolipa pindi tutakapokamilisha kukusanya taarifa kutoka kwa vituo vyetu,” alieleza.
Machi 9, mwaka huu Tanesco ilitoa notisi ya siku 14 kwa wateja wake
wote wanaodaiwa kulipa madeni yao, vinginevyo litawakatia huduma ya
umeme wateja wote sugu wanaodaiwa na shirika hilo.
Shirika hilo linadai jumla ya Sh bilioni 275.38 na makundi
yanayodaiwa ni pamoja na Wizara na Taasisi za Serikali zinazodaiwa zaidi
ya Sh bilioni 52.53, Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) linalodaiwa zaidi
ya Sh bilioni 127.87 na kampuni binafsi pamoja na wateja wadogo ambao
deni lao ni zaidi ya Sh bilioni 94.97.
Hata hivyo, tayari Serikali ya Zanzibar kupitia ZECO imeshapunguza
deni lake na kulipa kiasi cha Sh bilioni 10 huku Jeshi la Ulinzi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ) likiahidi kulipa kiasi cha Sh bilioni moja
kati ya zaidi ya Sh bilioni tatu linazodaiwa.
Hatua hiyo ya Tanesco kutoa siku 14 kwa wadaiwa wake sugu, imetokana
na agizo la Rais John Magufuli wakati akizindua ujenzi wa mradi wa
ujenzi wa kituo cha kupoza na kusambaza umeme wa kilovolti 132 mkoani
Mtwara ambacho kitaboresha upatikanaji wa umeme kwenye Mikoa ya Mtwara
na Lindi.
Katika agizo lake hilo kwa Tanesco alilitaka shirika hilo kuikatia
umeme hata Ikulu endapo haitalipa deni la umeme, ili kuliwezesha shirika
hilo kujiendesha zaidi.
chanzo:Mpekuziblog.
Comments