MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa
ataendelea kushirikiana na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Dk. John Pombe
Magufuli kama alivyofanya kwa Marais wastaafu Rais Benjamin William
Mkapa na Rais Jakaya Kikwete katika uongozi wao wakiwa marais Jamhuri ya
Muungao wa Tanzania.
Dk. Shein aliyasema hayo jana wakati akitoa salamu zake kwa Wajumbe
wa Mkutano Mkuu Maalum wa CCM, uliofanyika mjini Dodoma huko katika
ukumbi mpya wa Mkutano wa Kikwete.
Katika mkutano huo Dk. Shein, aliwahahakikishia Wajumbe hao wa
Mkutano Mkuu maalum kuwa ataendelea kufanya kazi kwa pamoja na
mwenyekiti huyo na kushirikiana nae katika kukitumikia chama hicho
pamoja na kuwatumikia wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani na pongezi kwa
Mwenyekiti wa CCM Taifa na kueleza matumaini yake makubwa aliyonayo
kutokana na uongozi wa Mwenyekiti huyo ndani ya chama hicho kikubwa na
kikongwe katika vyama vya bara la Afrika.
Aidha, Dk. Shein aliwaeleza wajumbe hao umuhimu wa kuendelea kufanya
kazi kwa kushirikiana kwa pamoja sambamba na kufuata kanuni na maadili
ya Chama.
Aliongeza kuwa kuna haja kwa wanaCCM wakaendelea na utamaduni wa
kuzipitia kanuni na maadili ya chama hicho ili kiendelee kupata
mafanikio makubwa zaidi.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alitoa pongezi na shukurani kwa wajumbe
wa mkutano mkuu maalum wa CCM kwa kukubali kwa pamoja mabadiliko ya
Katiba ya CCM kwa lengo la kukiimarisha na kukipa maendeleo zaidi chama
hicho.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
chanzo:zanzibar24.
Comments