Kutumika kwa wanawake hao ambao baadhi yao walikuwa na watoto wadogo
migongoni kumebainika jana wakati kamati hiyo ilipokuwa ikiendelea
kuangalia maeneo mbalimbali ya pori hilo tengefu la Loliondo lenye
ukubwa wa kilomita 15,000 za mraba zilizoleta mgogoro kwa zaidi ya miaka
25 sasa.
Wanawake hao katika Kata ya Malambo na Kata ya Arash, walibeba
mabango ya kuisihi kamati hiyo kutenda haki, huku mengine yakimtuhumu
Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe kuwapenda
wanyamapori kuliko binadamu.
Baadhi ya wanawake hao ambao ni Rehema Pascal na Lemnyaki John
walisimamisha msafara huo kwa kuonesha mabango yao yanayodai kutokubali
kuhamishwa katika pori hilo huku wengine wakipandisha mori na kupiga
mayowe.
Baada ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo kuyasoma mabango hayo
aliwapa vipaza sauti ili wayasome tena, hapo ndipo waliposhindwa
kuyasoma na kudai kuwa hawajui Kiswahili.
“Nani aliyewaandikia mabango haya wakati hamjui kusoma, mnatumiwa na
viongozi wenu kuhusu mgogoro huu, msikubali kutumika maana hamjui
serikali inafanya hivi kwa nia ipi na wala serikali haina mpango wa
kuchukua ardhi hii bali tunachokifanya ni kujua hayo mnayoyasema yapo
kiuhalisia au la ili tukamilishe kazi yetu,” alisema Gambo.
Naye Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Felix Wandwe, aliwataka
wananchi wa kata saba za wilaya hiyo kutokubali kutumika vibaya kwa
ajili ya pori hilo, kwani serikali inachofanya hivi sasa ni kuchukua
mapendekezo ya kamati hiyo kisha kuyawasilisha kwa Waziri Mkuu, Kassim
Majaliwa.
Pia, Katibu wa Kamati hiyo, Bahati Chisanza, alisema kuwa ni vyema
wananchi wakajua kuwa serikali haichukui ardhi bali inachokifanya ni
kutaka kupanga matumizi bora ya ardhi ili kila mtu anufaike nayo.
Awali, Mwenyekiti wa Kijiji cha Malambo, Lazaro Mashele alitoa rai
kwa kamati hiyo kutoiingiza kata hiyo ya Malambo katika matumizi bora ya
ardhi, kwani kata hiyo haina mgogoro na pori hilo bali ni wahifadhi
wazuri wa wanyamapori ingawa kata hiyo ni sehemu ya mazalia ya wanyama.
“Tunawaomba wakuu kata hii isiingizwe katika mgogoro huu kwani hatupo
ndani ya vijiji saba lakini pia kata hii inatumika kwa ajili ya mazalia
ya wanyamapori ambao hatuna ugomvi nao”.
Kwa upande wake, Gambo alisisitiza kuwa kamati hiyo imechukua maoni
ya mwenyekiti huyo na watafanyia kazi maoni yote yaliyotolewa na
wananchi, wahifadhi na wataalamu wa ardhi kisha kuyawasilisha kwa Waziri
Mkuu Machi 25, mwaka huu.
chanzo:Habarileo.
Comments