Wawili hao ambao ni wakazi wa Kijiji cha Katambike katika Kata ya
Ugala wilayani Mpanda mkoani Katavi, wamelazwa katika Hospitali ya
Manispaa ya Mpanda kwa matibabu.
Akizungumzia mkasa huo, Diwani wa Kata ya Ugala, Halawa Malendeja
alisema shambulio hilo lilifanyika juzi saa 12 alfajiri, baada ya chui
kuiingia kwenye zizi la ng’ombe nyumbani kwa Joseph Maiko ambaye ni baba
mzazi wa wawili hao.
“Baada ya chui huyo kuingia zizini alimshambulia ndama wa ng’ombe,
akiwa katika harakati ya kuondoka na ndama huyo ili akamle nje ya zizi
hilo…. ndipo Njamila aliposikia purukushani hizo zilizomsukuma atoke nje
ya nyumba alimokuwa amelala na kwenda kwenye eneo la tukio na
kushuhudia chui huyo akitaka kutoka nje ya zizi hilo akiwa na ndama
huyo,” alieleza Malendeja.
Aliongeza kuwa ndipo Njamili alipoingia zizini na kuanza kumshambulia
chui huyo kwa rungu na mnyama huyo alimwachia ndama aliyekuwa
anamburuza ili amtoe nje ya zizi hilo na kuanza kumshambulia Njamili
ambaye alipoona amezidiwa, alianza kupiga mayowe akiomba msaada.
Inadaiwa kuwa kaka yake Njamili, Maiko alisikia mdogo wake akipiga
kelele akiomba msaada ndipo alipotoka nje ya nyumba kwenda eneo la tukio
akiwa na rungu mkononi.
“Maiko aliingia zizini na kuanza kumshambulia chui huyo kwa rungu ili
kumuokoa mdogo wake …..
mnyama huyo alimwacha mdogo wake akiwa tayari
amemjeruhi vibaya mkono wake wa kulia uliokuwa ukivuja damu nyingi na
kumrukia Maiko na kumuuma shavu la kulia na kumjeruhi vibaya,” aliongeza
diwani.
Kwa mujibu wa diwani huyo, Maiko licha ya kung’atwa shavuni,
alionesha ujasiri mkubwa kwa kuikamata miguu ya mbele ya mnyama huyo na
kumwangusha chini na kuendelea kumshikilia.
Wakati akiendelea kupambana na chui, Njamili aliendelea kupiga mayowe
kwa kwa nguvu, ndipo majirani walipofika na kumuua chui huyo.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi, Damas Nyanda akithibitisha
kutokea kwa shambulio hilo na alieleza kuwa majeruhi hao wawili
walikimbizwa na kulazwa katika Zahanati ya Ugala kwa matibabu, ambako
walipatiwa huduma ya kwanza kisha wakahamishiwa Hospital iya Manispaa ya
Mpanda kwa matibabu zaidi.
Akizungumza akiwa hospitalini, Njamili alidai kuwa chui huyo alikuwa
dume, na licha ya kumparua sehemu mbalimbali za mwili wake, pia
alimjeruhi vibaya mkono wa kulia.
chanzo:Habarileo.
Comments