Msambazaji umeme wa REA Singida asitishwa kazi.

Mkurugenzi Mkuu wa REA, Gissima Nyamo-HangaWAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umesitisha mkataba wa mkandarasi Spencorn Services aliyekuwa akitekeleza mradi wa kusambaza umeme vijijini awamu ya pili kwa Mkoa wa Singida.

Mkurugenzi Mkuu wa REA, Gissima Nyamo-Hanga aliyasema hayo hivi karibuni katika hafla ya uzinduzi wa mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu katika Mkoa wa Singida uliofanyika kijijini Mkwese wilayani Manyoni.


Nyamo-Hanga alimweleza mgeni rasmi katika uzinduzi wa mradi huo, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kuwa, ufanisi wa kazi wa mkandarasi husika haukuwa mzuri hivyo kusababisha baadhi ya vijiji ambavyo vilipangwa kupelekewa umeme katika REA II, kutofikiwa na huduma hiyo.

“Tumechukua hatua za kinidhamu. Tumemsimamisha kazi na tutaleta wakandarasi wapya ambao wataendelea na kazi ya kusambaza umeme pale alipoishia,” alieleza mtendaji huyo wa REA.

Aidha, alitoa shukrani kwa serikali kwa ushirikiano na msaada ambao imekuwa ikitoa, ulioiwezesha REA kuendelea na kazi ya kuwafikishia umeme wananchi wa vijijini kwa mafanikio makubwa.
 chanzo:Habarileo.

Comments