Mifuko ya hifadhi ya jamii kuimarisha sekta ya viwanda Nchi..

MIFUKO ya Hifadhi ya Jamii nchini inatarajia itajenga viwanda 27 katika maeneo mbali mbali ya Nchi na kutarajia kuzalisha ajira 113,000 kwa Watanzania  kabla kufikia mwaka 2018.
Kauli hiyo kuwekeza katika ujenzi na ufufuaji wa viwanda nchini ilitolewa na Mwenyekiti wa Shirikisho la Mifuko ya Hifadhi Nchini (TSSA),
Eliud Sanga wakati wakihitimisha mkutano wa pili kuhamasisha ujenzi wa viwanda hivyo.
“Mifuko hiyo PPF, PSPF, LAPF, GEPF na NHIF imejizatiti kuwekeza katika kujenga viwanda 27 katika maeneo mbalimbali nchini ambavyo vitakamilika mwishoni mwa mwaka ujao na vitazalisha ajira 113,000,” alisema Sanga.
Sanga, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa LAPF alisema, mkutano wa kwanza ulifanyika Septemba 3, mwaka jana ambapo wakurugenzi wa mifuko waliefanya kazi ya kuandaa taarifa ya uwekezaji wao na mkutano wa tatu, hautafanyika ofisini bali kwenye maeneo ambayo viwanda vinajengwa ili kujiridhisha na ujenzi wake.
Mkutano huo wa pili, uliitishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu, Jenista Mhagama na kuratibiwa na Katibu wa TSSA, Meshark Bandawe, kupata taarifa ya uwekezaji wa mifuko hiyo.
Akifafanua kuhusu uwekezaji huo, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Profesa Godius Kahyarara alisema,
mfuko wake tayari umeshafanya uwekezaji kwa kukamlisha uzalishaji wa majaribio wa mradi viuadudu kilichopo Kibaha ambao kitazalisha ajira za moja kwa moja 150.
“Kiwanda cha viuadudu cha Kibaha kilianza uzalishaji wa majaribio kabla ya kuanza mwaka huu, kwa kutumia malighafi za hapa nchini na tayari kimesafirisha tani 100,000 za dawa hizo kwenda kuuzwa Niger,” alisema Profesa Kahyarara.
Alisema baada ya uwekezaji wa mtaji wa dola za Marekani milioni 2.1 kiwandani hapo uzalishaji kwa dawa za kuua mazalia ya mbu umeanza kwa asilimia 100 na kinasafisha bidhaa hiyo nje ya nchi.
Profesa Kahyarara alisema, NSSF pia imewekaza katika kilimo cha miwa na kiwanda cha sukari Mkulazi, Ngerengere mkoani Morogoro kwa kushirikiana na PPF ambacho kitazalisha ajira takribani 100,000.
Alisema, mfuko huo pia umewekeza katika kilimo cha miwa na kiwanda cha sukari huko Mbigiri mkoani Morogoro kwa kushirikiana na PPF na pamoja Jeshi la Magereza ambacho kitazalisha ajira 290.
chanzo;zanzibar24.

Comments