Mashirika ya umma yabanwa.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji Mitaji ya Umma (PAC), Albert NtabalibaKAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji Mitaji ya Umma (PAC) imeyataka mashirika ya umma 265 nchini, kuanza kujiandaa kuchangia bajeti ya serikali kuanzia mwaka ujao wa fedha.

Aidha, wakurugenzi na wenyeviti wa bodi wa mashirika hayo kuanzia mwakani watatakiwa kuwasilisha bajeti zao bungeni ili kupitishwa na Bunge na hakuna shirika lolote la serikali litakaloweza kupitishwa bajeti bila kuidhinishwa na Bunge.


Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo, Albert Ntabaliba wakati kamati hiyo ilipotembelea miradi ya Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (AICC) na kujionea miradi mbalimbali inayoendeshwa na kituo hicho, ikiwemo ujenzi wa nyumba za kupangisha, hospitali na jengo la maonesho na mikutano linaloendelea kujengwa na kituo hicho.

Ntabaliba alisema licha ya mashirika hayo kuwa na thamani kubwa ya Sh trilioni 26, lakini yamekuwa hayachangii ipasavyo bajeti ya serikali, hivyo yanatakiwa yabadilike na kuanza kulipa kodi ipasavyo pamoja na kutoa gawio serikalini.

“Mashirika yote ya umma yaliyopo nchini yana thamani ya shilingi trilioni 26 na kwa mwaka yamekuwa yakitoa faida ya shilingi bilioni 450 pekee, ambayo ni sawa na asilimia 1.08 kitu ambacho hakiwezekani ukilinganisha na mtaji uliopo wa trilioni 26, na hivyo wakurugenzi na wenyeviti wa bodi wametakiwa wahakikishe mapato yao kwa serikali yanapanda na angalau waweze kuchangia trilioni mbili kwa mwaka,” alisema Ntalibaliba.

Akizungumzia AICC, alipongeza miradi inayoendeshwa na kituo hicho na kushauri waanze kuchukua hatua ya kuanza kukabiliana na soko na pia wajitahidi kuwekeza zaidi katika ujenzi wa vituo vya mikutano vya kisasa na kuwataka kuelekeza nguvu zaidi ya kujenga kituo kikubwa cha mikutano katika mji mkuu wa Tanzania ambao ni Dodoma.

Hata hivyo, mmoja wa wabunge wa kamati hiyo, Ester Bulaya alikosoa gharama za ukarabati zilizotumika kukarabati Ukumbi wa Simba katika kituo hicho ambao kiasi cha Sh bilioni tatu na nusu zilitumika jambo ambalo hawakuafiki na kushauri kwamba fedha hizo ni nyingi sana na zingeweza kutumika kwenye uwekezaji mwingine.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa AICC, Elishilia Kaaya alisema amefurahishwa na ujio wa kamati hiyo kuwatembelea na pia wamekutana nao na wamepewa elimu nzuri ya uwekezaji na wametazama baadhi ya mambo yale ambayo hayajaenda sawa wamewarekebisha pale ambapo awapo vyema wamewafundisha hivyo wanaamini walivyoambiwa mtazamo ubadili utabadilika kulingana na hali ilivyo.

Hata hivyo, alisema kwa sasa wameanzisha mradi ujenzi wa kumbi za mikutano, mahoteli na maonesho unaogharimu Sh bilioni 2.8, ambao unatarajiwa kukamilika Mei mwaka huu, ambapo wanategemea utasaidia kuongeza mapato ya kituo hicho pamoja na ajira kwa Watanzania.
chanzo:Habarileo.

Comments