Masauni ataka ushirikiano kunasa wahalifu.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni.NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni amewataka wananchi wa wilaya za Kibiti, Rufiji na Mkuranga mkoani Pwani kuwapa taarifa za matukio ya uhalifu Jeshi la Polisi bila woga wowote ili jeshi hilo liwasambaratishe wahalifu katika maeneo hayo.

Masauni alisema jeshi hilo ili lifanikiwe katika mapambano yake na wahalifu , nguvu ya wananchi inahitajika sana katika utoaji wa taarifa ya matukio hayo.


Akizungumza na mamia ya wananchi wa Kijiji cha Bungu wilayani Kibiti, Masauni alisema jeshi hilo limejipanga kikamilifu kwa kupambana na wahalifu na litahakikisha wahalifu hao wanakamatwa wote ili wakazi wa maeneo hayo kuendelea kufanya shughuli zao za kuijenga nchi kama kawaida bila wasiwasi wowote. Hata hivyo aliwahakikishia usalama wananchi waendapo watatoa ushirikiano kwa jeshi hilo.

“… ili amani hii iweze kudumu, mnatakiwa kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi pale ambapo mnakuwa na taarifa na wasiwasi na mtu yeyote katika maeneo yenu ambaye hana nia nzuri na usalama wenu,” alisema Masauni.

Alisema Jeshi la Polisi halipaswi kuogopwa na raia mwema, ni rafiki kwa kila Mtanzania mwema ambaye ana uzalendo wa dhati na nchi yake, jeshi ni rafiki ya wananchi, hivyo wananchi wanapaswa kuwa karibu na Jeshi kwa kuwa hao ndio walinzi wa wananchi pamoja na mali zao.
chanzo:Habarileo.

Comments