Kipindupindu chatishia maisha ya watu Zambia, shule zafungwa kwa kuhofia maambukizi.

Wizara ya Afya ya Zambia imetangaza kuwa, ugonjwa wa kipindupindu umeenea katika maeneo ya kaskazini mwa nchi hiyo na kuwaathiri makumu ya raia.

Msemaji wa Wizara ya Afya ya Zambia amesema kuwa maafisa wa wizara hiyo wamewataka wananchi kutilia maanani usafi na taratibu za kinga ili kuzuia maambukizi zaidi ya ugonjwa wa kipindupindu. 


Ameongeza kuwa, watu walisiopungua 70 wameambukizwa ugonjwa huo na kwamba kuna uwezekano ukaenea zaidi katika maeneo mengine.

Wakati huo huo serikali ya Zambia imetangaza kwamba imefunga shule kadhaa na vituo vya uvuvi katika mkoa Luapula ili kuzuia maambukizi ya kipindupindu.

Waziri wa Afya wa Zambia, Chitalu Chilufya amesema kufungwa kwa shule hizo ni sehemu ya hatua za kudhibiti mlipuko wa kipindupindu katika mkoa wa Luapula ambapo makumi ya kesi za ugonjwa huo zimeripotiwa katika wiki nne za hivi karibuni.

Hali duni ya usafi na mazingira machafu vinatajwa kuwa sababu ya mlipuko wa kipindupindu katika maeneo yenye watu wengi nchini Zambia.

Ripoti iliyotolewa jana na UNICEF kwa mnasaba wa Siku ya Maji Duniani imeonyesha kuwa, watoto zaidi ya 800 wanapoteza maisha kila siku katika sehemu tofauti za dunia kutokana na ugonjwa wa kipindupindu unaosababishwa na mazingira machafu na ukosefu wa maji safi ya kunywa.
chanzo: parstoday.

Comments