Dkt Shein: TANESCO wakizima umeme tutawasha vibatari vyetu.

sheinRais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein amesema serikali yake haitishiki na tamko TANESCO la kukatiwa umeme na kwamba wapo tayari kutumia vibatari umeme ukikatwa.

Dkt. Shein aliyasema hayo katika mkutano wake na waandishi wa habari katika uwanja wa ndege wa Zanzibar mara baada ya kurejea kutoka Indonesia ambapo alisema kuwa deni hilo la TANESCO limekuwepo kwa miaka mingi na kwamba si la jana wala leo, hivyo kama umeme utakatwa wao watatumia vibatari.


“Tungoje basi uzimwe kama nyie muna wasiwasi, mimi najua hawezi kuuzima, kwa sababu deni hatujaanza kudaiwa leo sisi. Miaka 20 imepita tunadaiwa, kwahiyo mimi sitaki niseme sana leo kwenye hili na kama watazima basi, tutawasha vibatari vyetu, hatuna tatizo sisi. Lakini sidhani Tanzania iliyomakini kama inaweza kufanya vitu kama hivyo na sina uhakika kama magazeti yameandika vizuri,” alisema Dkt. Shein.

Aidha, Dkt Shein alisema haamini kama umeme utakatwa na kwamba pengine waandishi wa habari ndio waliokosea kuandika habari hiyo, lakini alisema yeye kama Rais wa Zanzibar atahakikisha deni hilo linalipwa.

TANESCO ilitoa siku 14 kwa wateja wake wote linalowadai kulipa madeni yao, vinginevyo litasitisha utoaji wa Huduma ya Nishati kwa wahusika.

Akifafanua zaidi Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka alisema, Wizara na Taasisi za Serikali zinadaiwa zaidi ya Shilingi Bilioni 52.53, Shirika la Umeme Zanzibar, (ZECO), linadaiwa zaidi ya Shilingi Bilioni 127.87, na Makampuni binafsi na Wateja wadogo wadogo deni ni zaidi ya Shilingi Bilioni 94.97.

chanzo: zanzibar24.

Comments