Bunge lataka maji Dodoma yapatikane kwa saa 24.

Sehemu ya Mji wa DodomaKATIKA kuhakikisha dhima ya serikali kuhamia Dodoma inakamilika, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imeitaka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Dodoma (Duwasa) kuongeza muda wa kupatikana maji kwa wateja kwa saa 24.

Taarifa ya Duwasa kwa kamati hiyo ilipotembelea miradi ya mamlaka hiyo juzi mjini hapa, inaonesha kuwa mamlaka hiyo imeboresha huduma za upatikanaji wa maji kutoka wastani wa saa 16 kwa siku hadi saa 22. 


Kamati imetaka yapatikane kwa saa 24.

Aidha, mamlaka hiyo imetakiwa pia kutekeleza agizo la Rais John Magufuli kwa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuwakatia umeme wadaiwa sugu, kwa wao (Duwasa) kuzikatia maji taasisi zote wadaiwa sugu zikiwemo za serikali.

“Sasa serikali inahamia Dodoma, maji yanatakiwa kupatikana kwa saa 24 na si 22 tena,” alisema mjumbe wa kamati hiyo, Mbunge wa Tanga Mjini, Mussa Mbarouk (CUF).

Mbarouk aliipongeza Serikali ya Awamu ya Nne chini ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete kwa kuhakikisha huduma ya maji inaboreka mkoani Dodoma ingawa yapo maeneo bado katika mkoa huo yanahitaji nguvu ya ziada.

“Sasa hata msikitini maji yanapatikana, namuomba Mwenyezi Mungu amlipe JK (Rais mstaafu Jakaya Kikwete) kwa hili,” alisema Mbarouk na kutoa dua hiyo kwa Rais mstaafu Kikwete.

Naye Mbunge wa Viti Maalumu, Yosefa Komba (Chadema) aliitaka Duwasa kuhakikisha mji wa Dodoma unapata maji katika kata zote na maeneo ya pembezoni kwa kuwa mkoa unatanuka kutokana na serikali kuhamia huko.

Kuhusu kuzikatia maji taasisi zilizo wadaiwa sugu, Mbarouk alisema agizo la Rais Magufuli alilolitoa kwa Tanesco, lihamie katika maji. 

Mkurugenzi wa Duwasa, David Pallangyo alisema mamlaka inapokea ushauri wa kamati na itachukua hatua.
chanzo:Habarileo.

Comments