Bodi yataka dola kusimamia sheria ya ujenzi.

Mwenyekiti wa AQRB, Dk Ambwene MwakyusaMWENYEKITI wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Ujenzi (AQRB), Dk Ambwene Mwakyusa amewaomba makamanda wa polisi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa kusimamia Sheria Namba 4 ya Mwaka 2010 inayohusu masuala ya ujenzi.

Akizungumza katika mkutano wa mashauriano kati ya Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo, Wakadiriaji Ujenzi pamoja na Jeshi la Polisi, Dk Ambwene alisema Sheria Namba 4 ya Mwaka 2010, inaitaka bodi yao iwe inasajili na kuratibu mienendo ya wabunifu majengo.


Alisema bodi yao imepanga kukagua miradi 1,800 ya ujenzi nchi nzima mwaka huu, baada ya mwaka jana kukagua miradi 1,227 na kwamba, watachukua hatua mbalimbali kwa miradi iliyokiuka sheria, ikiwa ni pamoja na kusimamisha shughuli za ujenzi.

“Bodi ina jukumu la kuingia na kukagua miradi ya ujenzi ili kuhakikisha imebuniwa na inasimamiwa na wataalamu waliosajiliwa. Hadi sasa Bodi yetu imesajili watalamu 1,442 na makampuni 393,” alisema.

Alimwomba Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Nsato Marijani aendelee kuwahimiza wataalamu wa ujenzi waliosajiliwa kuhudhuria mafunzo mbalimbali yanayoandaliwa na bodi hiyo.

Kwa upande wake, Kamishna Marijani aliipongeza AQRB kwa juhudi za ukaguzi wa maeneo ya ujenzi katika mikoa yote nchini.

Alisema Jeshi la Polisi nchini litaendelea kusimamia sheria hiyo na ameiomba AQRB kuhakikisha wanatoa ushirikiano kwa polisi pale wanapohitajika.
chanzo:Habarileo.

Comments