Zarif: Marekani iache kutoa vitisho dhidi ya Iran.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Muhammad Javad Zarif amesema hatua ya Marekani ya kutaka kuiwekea vikwazo vipya Iran inalenga kuichochea Tehran, na ameitaka nchi hiyo iache kutoa vitisho dhidi ya taifa hili.

Zarif ameyasema hayo katika mahojiano na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) na kusisitiza kuwa kuiwekea vikwazo vipya Iran kutakabiliwa na jibu mkabala la Jamhuri ya Kiislamu.


Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema Iran haijaanzisha wala haitoanzisha uhasama na wala haina mpango wa kuanzisha uadui dhidi ya nchi yoyote.

Amesisitiza kuwa itakachofanya kila mara Iran ni "kujihami"; na mpango wake wa makombora pia ni mpango wa "kujihami".

"Makombora ni wenzo wetu wa kiulinzi…Iran haina nia ya kuichochea nchi yoyote ile", amesisitiza Zarif.

Kuhusu matamshi yanayotolewa na maafisa wa Marekani, Israel na Saudi Arabia dhidi ya Iran, Waziri Zarif amesema: "Ninawataka waheshimu sheria za kimataifa na pia wakae watafakari wasije wakajitumbukiza kwenye matatizo makubwa".
Katika mahojiano mengine aliyofanyiwa na kanali ya televisheni ya NBC, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amefuta uwezekano wa kufanyika mazungumzo mengine na nchi zinazounda kundi la 5+1 kuhusiana na makubaliano ya nyuklia ya Iran.
Huku akisisitiza kuwa makubaliano ya nyuklia ya JCPOA yatadumishwa, Dakta Zarif amesema endapo Marekani itachukua hatua ya upande mmoja ya kujitoa kwenye makubaliano ya nyuklia, Iran nayo inayo machaguo kadhaa mezani ya maamuzi ya kuchukua…
chanzo:parstoday.

Comments