Zanzibar, Omani kuimarisha udugu wao.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Zanzibar itaendelea kuwa mshirika mkubwa wa Oman kutokana na historia ya miaka mingi iliyopo ya udugu wa kidamu baina ya Wananchi wake.

Alisema Oman imejitolea kwa nguvu zake kuunga mkono harakati za maendeleo na uchumi za Zanzibar kupitia udumishwaji wa ushirikiano huo ulioasisiwa na Viongozi wakuu wa pande hizo mbili.


Balozi Seif Ali Iddi alieleza hayo wakati akibadilishana  mawazo na Balozi Mdogo Mpya wa Omar aliyepo Zanzibar  Dr. Ahmed Humoud Al – Habsi aliyefika kujitambulisha rasmi Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.

Alishauri ziara za kukuza ushirikiano wa pande hizo mbili kwa kujumuisha Maafisa wa Taasisi, mashirika na hata jumuiya za kiraia uendelee kuimarishwa zaidi badala ya kuziachia ziara za sehemu hizo kufanywa na Viongozi wakuu pekee.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliipongeza Serikali ya Oman chini ya Utawala wa Mfalme Qabous  Bin  Said  kwa misaada mbali mbali ya maendeleo inayotowa kwa Zanzibar.

Balozi Seif aliutolea mfano msaada mkubwa wa Kiwanda cha Uchapaji Maruhubi kilichopata msukumo wa vifaa vya kisasa vilivyogharamiwa na Serikali ya Oman ambao ni hazina kubwa kwa Zanzibar.

Alisema miundombinu ya kisasa ya vifaa vilivyofungwa kwenye Kiwanda hicho cha Uchapaji itawezesha kazi zote za Serikali, Taasisi na Mashirika yake  hivi sasa kuchapishwa katika kiwanda hicho.

Akigusia suala la Mafuta na Gesi Asilia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimuomba Balozi huyo Mdogowa Oman aliyepo Zanzibar  Dr. Ahmed kuyashawishi Makampuni ya Nchi yake kufikiria wazo la Zanzibar katika kutaka kuwekeza kwenye Sekta hiyo Mpya.

Alisema Zanzibar hivi sasa iko mbioni kujiandaa na uanzishaji wa miradi ya Kiuchumi kupitia sekta ya Mafuta na Gesi ambayo Oman inaweza kusaidia Taaluma kwa vile Nchi hiyo tayari imekuwa mzalishaji mkubwa wa Nishati hizo kwa muda mrefu.

Naye Balozi Mdogo Mpya wa Oman aliyepo Zanzibar Dr. Ahmed Humoud Al – Habsi alimuahidi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Nchi yake itaendelea kushirikiana na Zanzibar katika kuona uhusiano wa kidugu uliopo baina nchi mbili unazidi kuimarika.

Alisema ahadi iliyotoa Oman kwa Zanzibar katika kugharamia matengenezo makubwa ya Ujenzi wa  Jengo la Jumba la Ajabu Forodhani Mjini Zanzibar  itatekelezwa kama ilivyopangwa.

Alimfahamisha Balozi Seif  kwamba matayarisho ya utengenezaji wa Jengo hilo hivi sasa yako tayari na ameahidi kufuatilia mitakaba iliyofikiwa ili kuona kazi rasmi ya ujenzi huo inaanza bila ya kupoteza wakati.

Dr. Ahmed  Humoud Al – Habsi  anaiongoza Ofisi ya Ubalozi Mdogo wa Oman Zanzibar kufuatia  aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo Balozi Ali Abdalla Al – Rashid aliyefariki Dunia  ghafla mwezi Mei mwaka 2016  baada ya kusumbuliwa na tatizo la sindikizo la Damu { Blood Presure }.

Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alifanya ziara ya kulikagua jengo la Mashariki Hoteli liliopo Pembezoni mwa Skuli ya Msingi Forodhani Mjini Zanzibar.

Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uhifadhi wa Mji Mkongwe wa Zanzibar Said Sarboko Makarani alimueleza Balozi Seif  kwamba Serikali kupitia Wizara inayosimamia Ujenzi ililikabidhi jengo hilo kwa Mamlaka hiyo baada ya kukaa kwa zaidi ya miaka 25  bila ya kutumiwa.

Mkurugenzi Sarboko alisema matengenezo ya Miaka Miwili ya jengo hilo yalianza mnamo mwaka 1985 ambapo baadaye mwaka 1987 ikalikodisha kutumiwa kama Hoteli ya Kimataifa.

Jengo la Mashariki Palace Hoteli Restaurent lililokuwa likijuilikana kwa jina la East Wings ni miongoni mwa majengo ya asili yaliyomo ndani ya Mji Mkongwe wa Zanzibar ulio katika Urithi wa Dunia chini ya Usimamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni                   { UNESCO }.

Othman  Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
chanzo: zanzibar24.

Comments