Waziri Ndalichako asubiriwa kutoa muongozo kesi ya waliofukuzwa Chuo kikuu.

ndalichakoUAMUZI katika kesi ya uwakilishi kwa wanafunzi 316 kati ya 480 waliofukuzwa katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Joseph kwa madai ya kutokuwa na sifa za kudahiliwa kwenye vyuo vikuu nchini, unatarajiwa kutolewa baada ya Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako atakapotoa mwongozo.

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imezitaka pande zote mbili zinazohusika katika kesi hiyo namba 311 ya mwaka 2016 kufanya usuluhishi kabla ya kusikilizwa.

Mwakilishi wa Wizara ya Elimu, Anna Kalomo amedai mbele ya Jaji Rose Temba kuwa ili kutoa uamuzi mzuri katika shauri hilo ni lazima Waziri husika awepo kwa kuwa tayari viongozi wengine wametoa mwongozo hivyo anasubiriwa Waziri.

Hata hivyo, aliomba mahakama kuahirisha kesi hiyo hadi tarehe nyingine kwa ajili ya kumpatia muda Waziri kupitia shauri hilo na kutoa mwongozo.

Jaji Rose Feleshi aliahirisha kutolewa kwa uamuzi huo hadi Februari 15 mwaka huu kwa ajili ya kupokea mwongozo wa Profesa Ndalichako ili kesi hiyo ianze kusikilizwa kwa Jaji Elieza Feleshi.

Mbali na mwakilishi huyo wa Wizara, Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU), inawakilishwa na Wakili Rose Ruta, Wakili wa Chuo hicho ni Jerome Msemwa na Wakili wa wanafunzi hao, Emmanuel Muga.

Madai ya msingi katika kesi hiyo inadaiwa kuwa walalamikaji (wanafunzi) hao wanadai fidia ya miaka mitatu waliokaa chuoni hapo dhidi ya TCU na chuo hicho cha Mtakatifu Joseph.

Awali wakati wa kufungua kesi hiyo, wanafunzi hao waliwasilisha maombi kupitia wakili Muga wakiomba kibali cha kuwawakilisha wenzao mahakamani hapo pamoja na kusitisha masomo wakati kesi ya msingi ikiendelea kusikilizwa.

Muga alidai kuwa wanafunzi ambao watawawakilisha wenzao ni Innocent Peter, Ramadhan Kipenya, Oswald Mwinuka na Feith Kyando.

Uamuzi wa wanafunzi hao kukimbilia mahakamani unatokana na agizo la Waziri huyo, Joyce Ndalichako lililoeleza kuwa kutokana na tatizo la ufundishaji wa Stashahada ya Elimu (Sayansi, Hisabati na Teknolojia) wanafunzi wote wanaosomea elimu hiyo wanatakiwa kurejea nyumbani.

chanzo:zanzibar24.

Comments