Watumishi waovu Maliasili kukiona.

KATIBU Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Jenerali Gaudence Milanzi amesema kazi ya kuwatambua watumishi wote waliopo katika taasisi zilizopo chini ya wizara hiyo itafanyika ili kuwabaini wanaoshirikiana na majangili ili wachukuliwe hatua za kinidhamu na kiutumishi.

Ameonya kuwa kuwa askari yeyote aliyefukuzwa katika jeshi lingine haruhusiwi kujiunga na taasisi yoyote iliyo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuwa wengi wao wamebainika kuwa si waminifu na wanaweza kuitia doa wizara hiyo.

Milanzi ametoa onyo hilo jana wakati akifunga mafunzo ya wahitimu wa mafunzo wa kutoka katika mfumo wa kiraia kwenda Jeshi Usu kwenye Kituo cha Mafunzo kilichopo katika Makao Makuu ya Pori la Akiba la Rukwa – Lwafi wilayani Mlele katika Mkoa wa Katavi.

Mafunzo hayo ya mwezi mmoja yaliyowashirikisha askari viongozi 133 wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongo (NCCA). Katika hafla hiyo, wahitimu walikula viapo vya utii na kutunukiwa ngazi za kiuhifadhi ili wafanye kazi kwa kufuata mfumo wa Jeshi Usu.

Katibu Mkuu alisisitiza kuwa uajiri katika taasisi zilizo chini ya wizara hiyo utazingatia uzalendo, uaminifu ambapo anayeajiriwa awe na uwezo wa kufundishika na kuwa na uhusiano mzuri na wananchi.

Alisema kwa miaka ya hivi karibuni nidhamu ya kazi katika taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii imeporomoka kwa kasi kubwa inayoashiriwa na visa ambavyo sio vya kiaskari na kiutumishi.

Aliwataka wahitimu wa mafunzo hayo ambao ni viongozi wa askari wasaidie kurudisha nidhamu ya kazi kwa askari walio chini yao kwa kuwaelekeza mambo mazuri ya kujenga.

Alitahadharisha kuwa kwa sasa hivi za taifa na mapori yote yanakabiliwa na changamoto kubwa, ikiwemo uwindaji haramu wa wanyama wakubwa wakiwemo tembo na faru kwa ajili ya pembe na vipusa na uingizaji wa mifugo hifadhini.

Alisisitiza kuwa ni matarajio yake kuwa wahitimu hao baada ya kupata mafunzo hayo hifadhi za taifa nchini zitakuwa salama.

“Hili linategemea moyo wa uzalendo na ari ya kujituma kwenu kwa kutumia mbinu mlizopata kuhakikisha kuwa mnatatua changamoto zilizo katika maeneo yenu ya kazi,” alisisitiza.

chanzo:habarileo.

Comments