Samia mgeni rasmi Siku ya Nile.

Image result for samia suluhuMAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya 11 ya Siku ya Nile yaliyolenga kukuza uelewa kuhusu umuhimu wa ushirikiano baina ya nchi wanachama, masuala yanayotekelezwa na faida inayopatikana kutokana na matumizi bora ya rasilimali zako Bonde la Mto Nile.

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Gerson Lwenge aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho hayo yatakayofanyika kesho Dar es Salaam ambayo yatahudhuriwa na washiriki zaidi ya 600.


“Serikali kupitia wizara yetu itakuwa mwenyeji wa maadhimisho haya na yameandaliwa kwa ushirikiano na Nile Basin Initiative (NBI) ambao jukumu lao kubwa ni kusimamia na kuendeleza rasilimali za Bonde la Mto Nile kwa niaba ya nchi wanachama zipatazo 10,” alisema Lwenge.

Lwenge alizitaja nchi hizo kuwa ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Ethiopia, Sudan, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Misri.

Alisema Mto Nile ni miongoni mwa mito mikubwa duniani wenye urefu wa kilometa 6,695 unaoanzia Ziwa Victoria nchini na ni chanzo kikubwa cha maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, viwandani, kilimo cha umwagiliaji na kuzalisha umeme kwa wakazi wa nchi za bonde hilo.

Alisema kaulimbiu ya mwaka huu imelenga kuonesha umma umuhimu wa Mto Nile katika kuhakikisha usalama wa upatikanaji wa chakula, maji na nishati ya umeme kwa jamii nzima na kuonesha muingiliano uliopo katika sekta husika kwa lengo la kuondoa umaskini, kuboresha maisha ya jamii na kuleta maendeleo endelevu.

Alisema maadhimisho hayo yanatarajiwa kuanza kesho saa 2:30 asubuhi kwa maandamano yatakayoongozwa na Bendi ya Polisi kuanzia Viwanja vya Mnazi Mmoja hadi Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC) ambako maonesho na ufunguzi rasmi utafanyika.

Alisema maadhimisho hayo yatashirikisha watu mbalimbali zikiwemo sekta mbalimbali, taasisi za serikali, taasisi zisizo za kiserikali, wadau wa maendeleo na watu mashuhuri.
 chanzo:Habarileo.

Comments