
Waliohukumiwa ni Peter Kabi (45) na mkewe Leonida Kabi (46) ambao walihifadhi meno ya tembo kwenye jeneza na kufunika na bendera ya Taifa kuonesha kuwa wanasafirisha msiba wa askari kwenda Tarakea.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi ambaye pia aliamuru vipande 212 vya meno ya tembo kukabidhiwa kwa Mkurugenzi wa wanyamapori.
Hata hivyo, mahakama hiyo iliwatia hatiani washitakiwa hao wiki iliyopita ambapo upande wa mashitaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Paul Kadushi na Elia Athanas waliomba kuongeza shahidi mmoja ili kukazia hukumu hiyo.
Akielezea kuhusu adhabu, Wakili Kadushi alidai kifungu namba 11 cha Sheria ya Wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009, kinaelezea kuwa masharti ni lazima kwa mahakama kutaifisha nyara zinazohusika na kesi hiyo ikiwemo meno ya tembo na mifupa mitano ya tembo.
“Lazima kitu chochote kilichotumika kufanyika kwa kosa la jinai vitaifishwe ikiwemo nyumba ambayo mshitakiwa wa kwanza anamiliki na viwe chini ya Mkurugenzi wa Wanyamapori,’’ alidai Kadushi.
Ilielezwa katika tarehe isiyofahamika kabla ya Oktoba 27, 2012 katika maeneo mbalimbali ndani ya jiji la Dar es Salaam na Iringa, kwa pamoja washitakiwa waliunda kundi la uhalifu kwa ajili ya kukusanya na kuuza nyara za serikali ambazo ni vipande 210 vya meno ya tembo bila kibali.
chanzo:zanzibar24.
Comments