Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi
(CUF), Maalim Seif Sharif Hamad ameahidi kuwa chama chake kitahakikisha
kinaibomoa ngome yote ya CCM Pemba kwa kuwashawishi wanachama wake kukihama.
Hata hivyo, alipotakiwa kutoa
maoni yake juu ya kauli hiyo ya Maalim Seif jana, Naibu Katibu Mkuu wa CCM
Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema makamu huyo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
katika Serikali iliyopita hana uwezo wa kuidhoofisha CCM Pemba kwa kuwa chama
chake kina msingi imara na wananchi wake wanakikubali.
“Uwezo aliokuwa nao Maalim Seif
ni kufukuza viongozi ndani ya chama chake kazi anayoifanya kila siku,” alisema
Vuai.
Maalim Seif alisema hayo juzi
alipokuwa akitoa kadi kwa wanachama wapya 2,240 waliojiunga na CUF kutoka
maeneo ya Kiuyu Minungwini, Kilindini Mapofu na Tumbe Wilaya ya Micheweni,
Kaskazini Pemba akiwa katika ziara yake ya siku 1.
Mara baada ya kukabidhi kadi
hizo, aliwaambia wanachama hao wapya kwamba wapo huru kufanya jambo lolote
ambalo lipo kwa mujibu wa sheria na katiba ikiwamo kupiga kura na kuwania
nafasi waitakayo.
Alisema hakuna mwanachama mwenye
haki ya kikatiba ndani ya chama hicho atakayenyimwa haki hivyo kuwataka
wasirudi nyuma.
Alisema kazi kubwa ya chama hicho
hivi sasa ni mapambano dhidi ya dhuluma aliyodai ilifanywa na chama tawala
dhidi ya CUF katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Akizungumzia madai hayo, Vuai
alisema hakuna dhuluma yoyote iliyofanywa na CCM dhidi ya CUF katika uchaguzi
uliopita.
Wakizungumza mara baada ya
kuhamia CUF, wanachama hao walisema lengo la kujiunga na chama hicho kikubwa
cha upinzani visiwani imetokana na kuchoshwa na ahadi zisizotekelezeka.
Walisema ustahamilivu umewashinda
hivyo wameamua kujiondoa CCM bila ya kushurutishwa ili kuungana na walio
wengi katika kudai haki yao nchini.
Sharifa Kamis Ali ambaye alikuwa
Sheha wa Shehia ya Kiuyu kupitia CCM alisema pamoja na kufanya kazi hiyo kwa
muda mrefu, hakuna alichokipata.
Alisema ndani ya chama hicho
alikuwa anafanya kazi bila ya kujiamini huku faida kubwa ikiwa ni kwa viongozi
wakuu na kuwaacha wa chini wakihangaika na ulimwengu.
chanzo:Mwananchi.
Comments