Dr. Al-Zahar: Lengo la mkutano wa Intifadha wa mjini Tehran ni kuunga mkono muqawama.

Kiongozi mwandamizi wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS amesisitiza kuwa, lengo la Mkutano wa Intifadha ya Palestina unaoanza leo hapa mjini Tehran ni kuunga mkono muqawama na mapambano na kwamba, nchi nyingine za Kiislamu nazo zinapaswa kuchukua hatua katika njia hiyo.

Dakta Mahmoud al-Zahar alisema hayo hapo jana katika mahojiano aliyofanyiwa na Shirika la Habari la Mehr na kubainisha kwamba,
lengo la Iran la kuitisha mkutano wa kuunga mkono Palestina ni udugu wa Kiislamu wenye lengo la kuunga mkono muqawama na kadhia ya Palestina kwa ajili ya kukabiliana na wavamizi wa Kizayuni.

Kiongozi huyo wa ngazi za juu wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS amesema kuwa, Wapalestina hawatafumbia macho haki ya kuzirejesha katika umiliki wao ardhi zao na kwamba, kushindwa mazungumzo eti ya mapatano katika miaka ya hivi karibuni ni ishara ya umuhimu wa muqawama na mapambano kwa ajili ya kukabiliana na upanuzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi na uingiaji wa kijinai katika msikiti wa al-Aqswa.
Mkutano wa sita wa kimataifa wa kuunga mkono Palestina unafanyika leo na kesho hapa mjini Tehran kwa kuhudhuriwa na wageni 700 kutoka nchi 80 duniani. Wanafikra, wasomi na maspika wa Mabunge wa baadhi ya nchi za Kiislamu ni miongoni mwa washiriki wa mkutano huo wa siku mbili.
Mkutano wa kwanza wa kimataifa wa kuunga mkono Intifadha ya Palestina ulifanyika hapa jijini Tehran mwaka 1991.
chanzo:parstoday.

Comments