Dk. Shein awataka vijana washindane katika michezo na wala wasigombane.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  ameelezea umuhimu wa michezo na kusisitiza kuwa michezo hujenga udugu, umoja, mapenzi na mshikamano katika jamii na wala sio ugomvi na uhasama.
 
Dk. Shein ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, aliyasema hayo huko katika ukumbi wa CCM, Mkoa wa Mjini uliopo Amani mjini Zanzibar mara baada ya kukabidhi vifaa vya michezo kwa vijana kwa ajili ya maandalizi ya Ligi ya Mpira wa Miguu kwa Timu 18 za Unguja ikiwa ni kusherehekea miaka 40 ya kuzaliwa kwa CCM.


Katika hotuba yake Dk. Shein aliwataka vijana washindane katika mchezo huo na wala wasigombane kwani lengo la michezo pamoja na kuanzishwa  kwa mashindano hayo ni kujenga umoja baina yao.

Dk. Shein aliwataka vijana hao wacheze vizuri ligi hiyo ili kuendelea kukipa heshima na mapenzi chama chao cha CCM na kueleza kuwa Ilani ya chama hicho ina vifungu vinavyoeleza kutekelezwa kwa sekta hiyo ya michezo.

Aliongeza kuwa mashindano hayo yana lengo la kuimarisha chama, kutoa vipaji kwa vijana na kuwataka viongozi wa Majimbo kuwaunga mkono na kuwasaidia vijana wao watakaoshiriki katika ligi hiyo kwani na wao wanawajibu wa kufanya hivyo.

Pia, Dk. Shein  alikubali rai iliotolewa na Mwakilishi wa Jimbo la Uzini ambaye pia, ndio mdhamini wa mashindano hayo Mohammed  Raza ya kuanzisha mashindano kama hayo kisiwani Pemba pamoja na mashindano ya vijana katika skuli za Mikoa yote ya Zanzibar na kuahidi kuyadhamini kwa kushirikiana na wahisani wengine wa michezo hapa nchini.

Dk. Shein ambaye aliongeza  kuwa uzinduzi wa mashindano hayo utafanyika tarehe 24 mwezi ujao kati ya Timu ya Mfenesini na Mpendae mchezo utakaopigwa katika uwanja wa Amaan mjini Zanzibar.

Nae Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambaye pia, ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Balozi Seif Idd, alitumia fursa hiyo kueleza umuhimu wa mashindano hayo kwa vijana na kusisitiza kuwa ligi hiyo itazidi kukuza mashirikiano na umoja kwa vijana wa chama hicho.

Mapema Mdhamini wa mashindano hayo, Mohammed Raza alisema kuwa mchakato wa kuanzishwa kwa mashindano ya ligi hiyo ni miongoni mwa utekelezaji wa Ilani ya CCM sambamba na kutekeleza malengo ya kuwatumikia wananchi na utekelezaji wa ahadi kwa wananchi.

Raza alisema kuwa kazi kubwa iliyopo hivi sasa ni kuwatumikia wananchi bila ya ubaguzi na kusisitiza umuhimu wa mashirikiano ya pamoja kwa wanaCCM ili kufikia malengo waliyojiwekea huku akieleza azma yake ya mashindano hayo kuyapeleka kisiwani Pemba.

Katika taarifa ya Ligi hiyo iliyosomwa na Omar Suleimn, Mjumbe wa wa Kamati ya Michuano hiyo, ilieleza kuwa Umoja wa Vijana wa CCM kwa kushirikiana na CCM Mkoa wa Mjini, wameamua kuanzisha ligi ya Majimbo ya Mpira wa miguu ambayo itashirikisha timu 18, Timu 9 kutoka Majimbo ya Mkoa wa Mjini kichama, Timu ya Tawi la Afisi Kuu ya CCM, Timu ya CCM Family na Timu zilizo salia zitatoka Mkoa wa Magharibi, Kusini na Kaskazini Unguja.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa mara baada ya kupata wazo la kuanzisha ligi hiyo, iliundwa Kamati ya maandalizi ya mashindano hayo yenye Wajumbe 12 chini ya uongozi wa CCM Mkoa wa Mjini ambapo mshauri wa Kamati hiyo Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohammed Mahmoud.

Kwa maelezo ya taarifa hiyo lengo la mashindano hayo ni kusherehekea miaka 40 ya kuzaliwa kwa CCM, kuinua vipaji vya vijana katika mchezo wa mpira wa miguu sambamba na kuunga mkono kauli ya Dk. Shein ya kutaka Zanzibar iwe na vuguvugu la michezo kwani wanaamini kuwa hoja hiyo imelenga utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Vijana hao pia, walitoa salamu zao za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tazania John Pombe Magufuli kwa jitihada zake za kupambana na biashara haramu ya madawa ya kulevya.

Mshindi wa kwanza wa mashindano hayo atapata kikombe, gari na nishani ambapo mshindi wa pili atapata milioni tatu na mshindi wa tatu atapata milioni mbili pamoja na zawadi nyengine zitakazotolewa katika mashindano hayo.

Mbunge wa Jimbo la Mpendae  Salim Turky kwa upande wake akiwa pia, ni mkereketwa wa michezo hapa nchini aliahidi kununua gari hiyo kwa ajili ya mshindi wa kwanza wa mashindano hayo ambapo wafanyabiashara wengine na wakereketwa wa chama hicho waliahidi kuchangia mashindano hayo zikiwemo fedha taslim.

Miongoni mwa Timu zitakazoshiriki mashindano hayo ni Jimbo la Mpendae, Jangombe, Kikwajuni, Kwahani, Amani, Shaurimoyo, Chumbuni, Malindi, Magomeni, Kiembesamaki, Mfenesini, Dimani, Mahonda, Uzini, Kaskazini A, Kusini, Afisi Kuu ya CCM pamoja na timu ya CCM Family.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
 chanzo:zanzibar24.

Comments