Balozi wa Uturuki mjini Tehran aitwa Wizara ya Mambo ya Nje.

Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imemuita balozi wa Uturuki hapa mjini Tehran na kumkabidhi malalamiko rasmi kufuatia matamshi ya uingiliaji masuala ya ndani ya Iran yaliyotolewa na Rais pamoja na Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa nchi yake.

Ibrahim Rahimpoor, Naibu Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran anayehusika na masuala ya Asia na Ocenia jana alimuita Reza Hakan Tekin balozi wa Uturuki hapa mjini Tehran na kumkabidhi rasmi malalamiko
ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kutokana na matamshi yaliyotolewa na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan na waziri wake wa mashauri ya kigeni Mevlüt Çavuşoğlu dhidi ya taifa hili.
Akihutubia siku ya Jumapili katika mkutano wa usalama wa Munich Ujerumani, Mevlüt Çavuşoğlu Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Uturuki alidai kwamba, Iran inafanya njama za kuzifanya nchi mbili za Iraq na Syria ziwe za Kishia.

Aidha wiki moja kabla yake, Rais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki akihutubia katika taasisi ya kimataifa ya amani huko Bahrain alitoa tuhuma dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Erdogan aliashiria migogoro ya Mashariki ya Kati kama ya Syria na Iraq na kudai kwamba, katika nchi hizo kwa wakati mmoja kuna mjadala na mvutano wa kikaumu na kimadhehebu.

Katika kujibu matamshi hayo ya Rais Erdogan, Bahram Qassemi, msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Iran alisema kuwa, Bwana Erdogan anafahamu kuliko mtu mwingine yeyote nafasi muhimu ya Iran na yenye kuleta uthabiti katika Mashariki ya Kati hususan nchini Iraq na inaonekana Rais huyo alitoa matamshi hayo kwa kufuata mkumbo wa anga iliyokuwa ikitawala au yawezekana alitamka hayo kutokana na anga maalumu ya hamasa iliyokuwako mahala alipokuwa akizungumza.
chanzo:parstoday.

Comments