Serikali yavunja mkataba na kampuni ya ujenzi, yazuia mali.

 Mkuu wa Mkoa Kigoma, Emmanuel MagangaSERIKALI imevunja mkataba na kampuni ya SPENCON iliyopewa kandarasi ya mradi mkubwa wa maji uliokuwa ukitekelezwa katika Manispaa ya Kigoma Ujiji na kukwama baada ya kampuni hiyo kufilisika.

Mradi huo ulikuwa unafanyika kwa msaada wa serikali ya Ujerumani.

Mkuu wa Mkoa Kigoma, Emmanuel Maganga, akitoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo kwa mwaka 2016 amesema kuwa mradi huo ulipaswa kukamilika Machi mwaka huu na kwa hatua hiyo mradi huo hautaweza kukamilika kama ilivyokusudiwa.

Alisema kwa muda sasa mkandarasi huyo ameshindwa kuingiza pesa za kuendelea na hatua za utekelezaji wa mradi baada ya pesa alizokuwa akilipwa na kuingizwa kwenye akaunti yake kuchukuliwa na taasisi zinazoidai kampuni hiyo.

Pamoja na hatua ya kuvunja mkataba huo, serikali pia imezuia mali na mitambo yote ya kampuni hiyo.

Amewataka wananchi kuzuia mitambo katika maeneo ya miradi isiondolewe kwa namna yeyote.

Akielezea hali hiyo, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa Kigoma, Aziz Mutabuzi alisema kufuatia kufilisika kwa kampuni hiyo, Wizara ya Maji na Umwagiliaji imeanza kuchukua hatua kuona namna ya kutafuta mkandarasi wa kuukamilisha mradi huo.

Pia serikali inatarajia kununua pampu mpya kuongeza uwezo wa uzalishaji maji wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Kigoma/ Ujiji wakati taratibu nyingine zikiendelea.

Alisema ili kukamilisha mradi huo, kiasi cha sh bilioni 32 zinatarajiwa kutumika. Kwa sasa, mradi umetekelezwa chini ya asilimia 50.

chanzo;habarileo.

Comments