RC Dodoma afanikiwa kuzima mgogoro wa wakulima, wafugaji.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana.MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana, amezima mgogoro uliokuwa ukifukuta wa kugombea eneo baina ya wakulima na wafugaji katika kijiji cha Makanda, kilichopo katika kata ya Makanda wilayani Bahi, mkoani humo.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara kijijini hapo, Mkuu wa Mkoa, Rugimbana alisema, kijiji hicho kina mpango wa ardhi wa siku nyingi, hivyo ni vema ukazingatiwa na kufuatwa badala ya watu kuvamia maeneo kiholela.

Mkuu wa mkoa huo alisema, amri iliyotolewa na wakuu wa wilaya hiyo waliotangulia, inabaki vivyo hivyo, hakuna shughuli zozote kuendelea katika eneo hilo ambalo linagombaniwa hadi kamati iliyoundwa na wilaya ambayo mkoa utaongeza watu wake itakapokamilisha uchunguzi wake.

“Marufuku kufanya shughuli zozote katika eneo hilo, hadi kamati iliyoundwa na viongozi wa wilaya ambayo mimi nitaongezea watu, itakapokamilisha uchunguzi,” alisisitiza.

Alisema waliovamia maeneo hayo, kabla ya kuwaita wavamizi au kabla ya kuwachukulia hatua, wanatakiwa kujisajili kwa viongozi wa kijiji wanaohusika, kupitia mikutano ya hadhara, wasipofanya hivyo, watawahesabiwa kuwa ni wavamizi wa maeneo ya kijiji hicho na hawana nia nzuri.

Huku akishangiliwa na wananchi, Mkuu wa Mkoa alisema, maeneo hayo yamevamiwa na watu ambao sio wa kijiji au kata ya Makanda, wamechukua maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wafugaji na kuyabadili kuwa ya kilimo.

Akizungumza kwa msisitizo alisema, waliovamia maeneo hayo ni wahuni wachache kutoka nje ya eneo hilo, na kusababisha vurugu miongoni mwa wananchi na kuvuruga mpango ardhi wa kijiji kwa kutoa fedha kidogo ili kupata maeneo hayo.

Mkuu wa Mkoa aliwataka wazee wa kijiji hicho kumsaidia katika kuhakikisha amani inadumu kijijini hapo, akawataka kwanza waunde Baraza lao ili kusaidiana na madiwani katika kuhakikisha wanasimamia amani kijijini hapo.

Diwani mstaafu wa Kata ya Makanda, Anthony Lyamunda, alimsifu Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kufika kijijini hapo kwani wamekuwa wakisumbuliwa na watu wanaoitwa vishoka kutokana na vitendo vya kuvamia ardhi wanaotaka kubadili matumizi ya ardhi kijijini hapo.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Makanda, Msafiri Makacha, wakati akifunga mkutano huo, alimweleza Mkuu wa Mkoa kwamba kamati iliyoundwa na viongozi wa wilaya inaanza kazi leo (jana) kutatua mgogoro wa ardhi, ana hakika watapata ufumbuzi wa kudumu juu ya suala hilo.

chanzo:habarileo.

Comments