Mvua ya dakika 30 yaua mtoto, yabomoa nyumba 20.

MVUA kubwa iliyoambatana na upepo iliyonyesha kwa dakika 30 imesababisha kifo cha mtoto mmoja na watu wengine watano kujeruhiwa, huku ikibomoa nyumba zaidi ya 20 na vyumba vitatu vya Shule ya Msingi Idilo, wilayani Mpwapwa.

Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Jabir Shekimweri amethibitisha, akisema mtu huyo alikufa baada ya kuangukiwa na ukuta wa nyumba.

Amemtaja aliyekufa kuwa ni Msafiri Erasto (9), mkazi wa Lukole wilayani hapa. Aidha amewataja waliojeruhiwa kuwa ni Yared Msenzi (60) Siwatu Delela, Alex Delela na Tumayo Msenzi (50).

Mvua hiyo ilinyesha juzi Januari 3 na kwamba majeruhi ni watu wa familia moja.

Mkuu huyo wa wilaya ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama amesema kwamba majeruhi wanapatiwa matibabu katika Hospitali ya Benjamini Mkapa.

Aidha, amesema wameunda kamati ya tathmini kuona athari zilizosababishwa na mvua hiyo.

Naye Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa, Boniface Makiya alisema wanajipanga kurejesha vyumba vya madarasa katika hali ya kawaida ili viweze kutumika kuanzia jumatatu ijayo.

chanzo;habarileo. 

Comments