IDARA ya Maendeleo ya Uvuvi Kisiwani Pemba, imekabidhi
majembe matano (5), Mapauro kumi na tano (15), na shoka mbili (2),vikiwa na
thamani ya shilingi laki mbili na elfu sita (26000/=), kwa Wanaushirika wa
kikundi cha Ufugaji Samaki kinachojulikana kwa jina la ‘Nguvu Kazi’ ,kilichopo
Chamabani, Wilaya ya Mkoani.
Akikabidhi kwa niaba ya Waziri wa Wizara ya Kilimo,
Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Ofisa Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Uvuvi, Sharif
Muhammed Faki, amesema kuwa, vifaa hivyo vimetolewa kufuatia ahadi iliowekwa na
waziri wa wizara hiyo katika ziara zake za kikazi za kawaida.
Katika maelezo yake amewataka wanavikundi hao kuzidisha bidii
katika shughuli zao, kwa kuona kuwa nguvu zao zinazaa matunda na fursa ya
kupatiwa vifaa hivyo kama walivyokusudia.
Pamoja na hayo, amewasihi kuvitumia vifaa walivyopatiwa katika
shughuli za ufugaji wa Samaki na si vyenginevyo, ili kuongeza uzalishaji kwa
faida yao na Serikali kwa ujumla.
Hata hivyo, amewasisitiza uwekaji wa kumbukumbu kwa kikundi
hicho, ili kudhibiti taarifa sahihi za utekelezaji wa shughuli zao, ambazo
zitatambulika na kila mmoja wa ushirika
na hata kwa viongozi wanapozihitaji .
Kwa upande wake, Ofisa Ufugaji wa Viumbe vya Baharini Pemba,
Mohammed Salim Othman, alisema kuwa Serikali inajitahidi kuwapitia wananchi
wake kwa ajili ya kuona maendeleo ya shughuli zao, pamoja matatizo
yanayowakwamisha, ili waweze kujua ni jinsi gani ya kuwasaidia kila hali
inaporuhusu.
Wakati huohuo wanaushirika wa kikundi hicho, walitoa
shukurani zao kwa Waziri kwa kutekeleza ahadi alioiweka kupitia Idara hiyo, kwa
kuona umuhimu wa shughuli zao kwa kuwapatia vifaa muhimu katika utekelezaji wa
shughuli zao.
Nae Katibu wa kikundi hicho, Said Abrahman Juma, kwa niaba ya wanaushirika wenzake
ameahidi kuvitumia vifaa hivyo katika malengo yaliokusudiwa pamoja na uangalifu
mkubwa katika shughuli zao na kufikia malengo waliojiwekea na hata kufikia kuwa
kikundi bora katika ufugaji wa samaki kwa Mkoa.
Ushirika wa kikundi cha Ufugaji wa Samaki kinachojulikana kwa
jina la ‘Nguvu Kazi’, kilichopo Chamabani, Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba,
Kilianza shughuli zake Juni,21-2006, kwa wanachama 26 wakiwemo wanawake 12, na
wanaume 14.
Comments