Kampuni ya Orttelo yaweka mambo hadharani kwa RC.

 Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo
UONGOZI wa Kampuni ya Uwindaji ya Orttelo Business Corporation (OBC) inayomiliki Pori Tengefu la Loliondo, umeweka mambo hadharani mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo, ikieleza kuwa kila mwaka hutoa msaada wa Dola za Marekani 1,037,000 (Sh bilioni 2.8) kwa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro kwa ajili ya shughuli za maendeleo katika wilaya hiyo.

Mkurugenzi wa OBC, Issack Mollel alisema hayo baada ya kuelezea changamoto zinazowakuta katika utendaji kazi wa kila siku mbele ya kamati ya wataalamu kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, viongozi wa serikali ngazi ya halmashauri, wilaya na mkoa, madiwani wa halmashauri hiyo na viongozi wa mila na kijamii mwishoni mwa wiki.

Mollel alisema OBC haina ugomvi na jamii inayozunguka pori hususani vijiji vinane, lakini imekuwa ikilaumiwa kila kukicha kuwa haijafanya chochote kwa maendeleo ya vijiji hivyo wakati inatoa mamilioni ya dola kwa ajili ya maendeleo ya afya, maji, elimu na miundombinu ya barabara kwa kipindi chote akiwa mkurugenzi kuanzia mwaka 2006.

Alisema mbali ya kuilipa halmashauri mamilioni hayo ya dola kwa ajili ya maendeleo ya vijiji hivyo, pia OBC huilipa Serikali Kuu mamilioni ya dola kwa mujibu wa mkataba walionao tangu mwaka 1993.

Mkurugenzi huyo alisema baadhi ya viongozi ngazi ya wilaya, wamekuwa wakiwachonganisha na OBC na wananchi wa vijiji hivyo kuwa kampuni hiyo ya uwindaji katika muda wote huo, haijafanya chochote kwa ajili ya wananchi na kuikatisha tamaa wakati inatoa mamilioni ya dola, lakini hawataki kusema ukweli wa mgawo huo.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa sisi hatuna ugomvi na jamii na tunaishi nao vizuri sana na tunatoa misaada kwa hisani bila ya kusukumwa kila mwaka, lakini msaada huo unaonekana kama si lolote,” alisema Mollel na kuongeza: “Angalia kwa mwaka tunatoa kiasi hicho cha fedha cha dola za Marekani 1,037,000 na pia halmashauri na hupewa tena asilimia 25 ya mapato kutoka serikali kuu kwa kile tulicholipa kule hivyo kwa mwaka halmashauri hiyo hupata zaidi ya shilingi bilioni nne.”

Akizungumzia changamoto zinazowakabili katika hicho kilichohudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Wanyamapori nchini, Profesa Alexander Songoro, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (Tawiri), Dk Simon Mduma, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa), Allan Kijazi na Ofisa Misitu Mkuu, Nurdin Chauya, mkurugenzi huyo wa OBC alisema ni kuwa na wawekezaji wawili ndani ya pori hilo kinyume cha mkataba.

Wengine waliohudhuria kikao hicho ni pamona na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyama Pori Nchini (TAWA), Martin Loiboki, Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, ambaye ni mbunge wa Ngorongoro, William Ole Naasha, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, Lekule Laizer, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Dk Fred Manongi.

Mollel alisema kwa mujibu wa mkataba walionao, pori hilo halipaswi kuwa na wawekezaji wawili, lakini kwa sasa wana mwekezaji mwingine Kampuni ya And Beyond iliyoingia mkataba na Kijiji cha Ololosokwan kufanya shughuli za utalii wa picha na inalipa mamilioni ya fedha moja kwa moja kijijini, tofauti na wao wanaolipa halmashauri.

Alisema pamoja na mkanganyiko huo, kuripotiwa sehemu husika yaani serikalini, lakini wao wamekuwa wakiendelea kufanya kazi kwa ushirikiano kwa kupeana zamu za kuwinda na kupiga picha ili kusiweze kuleta madhara pindi wanapokutana mbugani.

Changamoto nyingine zinazowakabili ni pamoja na kuingiza mifugo kwa wingi kutoka nchini na nchi jirani ya Kenya na kuharibu kwa kiasi kikubwa uoto wa asili na kuharibu vyanzo vyote vya maji kwa asilimia kubwa na kufanya wanyama kuhama katika pori hilo.

Mollel alisema OBC inapendekeza kuwa taratibu na sheria za wanyamapori zinapaswa kufuatwa na kusimamiwa kikamilifu, ikiwemo matumizi bora ya ardhi, kuzuia mifugo kuingia katika pori hilo, kulinda kwa vyanzo vya maji kwa gharama yoyote na kutokomeza kilimo ambacho kinakuwa kwa kasi katika pori hilo bila ya sababu za msingi.

Diwani wa Kata ya Ololoswokani, Yannick Ndoinyo ambaye aliwakilisha mapendekezo ya jamii inayozunguka pori hilo, alisema mgogoro wa pori la Loliondo ulikua zaidi pale Waziri wa Maliasili na Utalii wakati huo, Dk Khamis Kagasheki alipotangaza kuwa kilometa za mraba 1,500 kuwa ni pori tengefu.

Ndoiyo alisema jamii inaona kuwa ufugaji na uhifadhi vinawiana pamoja, hivyo hawaoni kama kuna tatizo na kusema kuwa ikifanyika hivyo mgogoro huo utakuwa historia na malisho na kilimo kitambulike kisheria katika pori hilo tengefu la Loliondo.

Mtafiti Mkuu wa Taasisi ya Wanyamapori, Edward Koho alisema vyanzo vya maji vilikuwa vikipeleka maji katika Hifadhi ya Serengeti ambavyo viko katika Pori la Tengefu la Loliondo vimekufa kutokana na uharibifu wa mifugo na kilimo kikubwa kinachofanyika katika pori hilo kinyume cha sheria za uhifadhi.

Baada ya kusikiliza mapendekezo ya awali ya jamii, wawekezaji na wataalamu, Gambo alisema yatawakilishwa katika kamati na kufanyiwa kazi kabla ya kupelekwa kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kama alivyoagiza ili kumaliza mgogoro huo uliodumu kwa zaidi ya miaka 25.

chanzo;habarileo.

Comments