Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hafla ya uwekaji wa jiwe la
msingi la Hoteli ya Verde-Mtoni Marine, iliyopo Mtoni nje kidogo ya mji
wa Zanzibar inayomilikiwa na “Bakhresa Group of Companies”.
Dk. Shein alisema kuwa ni lazima wananchi washirikiane, waipende
nchi yao na kufanya kazi kwa bidii kwani kila mmoja ana nafasi akiwa
Zanzibar au nje ya Zanzibar ya kutoa mchango wake adhimu kwa ajili ya
kuijenga Zanzibar
Dk. Shein alitoa pongezi kwa Mwenyekiti wa “Bakhresa Group of
Companies”, Said Salim Bakhresa kwa umahiri, ari na ujasiri wake wa
kuyatekeleza kwa vitendo mambo anayoyaahidi, anayoyasema na anayoyaamini
sambamba na uzalendo alionao katika kushirikiana na Serikali pamoja na
wananchi katika kuijenga Zanzibar.
Hata hivyo Dk. Shein alieleza kuwa Serikali itaenda sambamba na
watendaji waliokuwa hawaiwezi kasi ya maendeleo iliyokusudiwa na
kusisitiza kuwa watendaji wazembe hawatovumiliwa hasa wale
wanaodhorotesha masuala ya uwekezaji.
Alieleza kuwa wawekezaji wanataka watu wakweli na hawataki
wababaishaji hivyo aliwasisitiza watendaji wote kufanya kazi zao kwa
ufanisi huku akisisitiza kuwa watakaoshidnwa kwenda na kasi hiyo watakaa
pembeni.
Pia, Dk. Shein alieleza faraja yake kutokana na hoteli hiyo kuja
kutoa ajira zaidi ya 1200 ambalo hilo ni jambo muhimu katika kipindi
hichi ambacho suala la ajira ni changamoto kwa vijana wa hapa nchini.
Alieleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kujitangaza
kiutalii, na jinsi idadi ya watalii inavyoongezeka sambamba na juhudi
zinazofanywa kati ya Serikali na mashirika ya ndege mbali mbali duniani
ili yafanye safari za kuja Zanzibar ambapo hivi karibuni Shirika la
Uturuki limeanza safari za kuja Zanzibar rasmi.
Dk. Shein alieleza umhimu wa kuwepo wka mashirikiano kati ya Serikali
na Sekta binafsi katika kukuza na kuutangaza utalii huku akisisitiza
suala zima la amani na utulivu nchini kwa faida ya kila mmoja na
kuwasihi wananchi kuimarisha amani na utulivu ili utalii uendelee kukua
hapa nchini.
Pia, alieleza haja ya kujidhatiti katika kuuimarisha utalii wa ndani
hapa Zanzibar kwani kuna vitu vingi ambavyo nchi nyengine havipo na
kutumia fursa hiyo kueleza kuwa ujenzi wa hoteli hiyo unatarajiwa
kukamilika mwezi wa sita mwaka huu.
Nae Waziri wa Fedha na Mipango Dk. Khalid Salum Mohammed alipongeza
hatua za makusudi zinazofanywa na Kampuni hiyo ya Bakhresa kwa
kushirikiana na Serikali katika kuimarisha sekta ya utalii ambayo ndio
inayoongoza katika kukusanya mapato.
Alieleza kuwa wananchi wanafarajika kwa kiasi kikubwa na juhudi za
Dk. Shein za kuleta maendeleo na kusema kuwa kukamilika kwa hoteli hiyo
kutachangia uchumi wa nchi sambamba na kutoa huduma kwa jamii ikiwemo
suala zima la ajira na kuahidi kuwa Wizara yake itaendeleza ushirikiano
na Kampuni hiyo katika miradi yake yote.
Nae Mkurugenzi wa Mamlaka ya Uwekezaji wa Vitega Uchumi Zanzibar
(ZIPA), Salum Khamis Nassor alieleza majukumu na shughuli za Mamlaka
hiyo na jinsi ilivyoshirikiana na Kampuni ya Bakhresa Group katika
kuanzisha mradi huo pamoja na na fedha zaidi ya Dola milioni 20
zitakazotumika hadi kukamilika kwake.
Mapema Mwakilishi wa Kampuni ya Bakhresa Group of Companies Salim
Aziz alieleza kuwa ujenzi wa hoteli hiyo ya kisasa ya kitalii ya hadhi
ya nyota tatno ambayo ni rafiki wa Mazingira unaendelea na itakuwa na
vyumba 106 vikiwemo 6 vyenye hadhi ya kutumiwa na Marais.
Aidha, alisema kuwa hoteli hiyo itakuwa ni ya kisasa kabisa na ya
kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na kupata usajili wa
kuwa na uhifadhi mkubwa wa Mazingira kwani itakuwa inatumia umeme wa
jua, mitambo maalum ya kurejesha maji yanayotumika hotelini na makasha
maalum ya kutenganisha aina za taka.
Hoteli hiyo itakuwa na ukumbi wa mikutano, michezo ya maji, eneo
maalum kwa ajili ya kuegesha boti za kitalii ambapo pia kutakuwa na boti
ndogo ndogo kwa ajili ya kwuapelekea watalii katika visiwa vya Prison
Islan na vyenginevyo pamoja na mambo mengineyom hoteli hiyo pia itakuwa
na uwezo wa kutumiwa na watu zaidi ya 2500.
Hafla hiyo ya uwekaji wa jiwe la msingi la hoteli hiyo ni miongoni
mwa shamra shamra za maadhinisho ya miaka 53 ya Mapinduzi matukufu ya
Zanzibar ya Januari 12, 1964 ambayo ilipambwa na ngoma za utamaduni,
taarab asili na utenzi.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
chanzo;zanzibar24.
Comments