Dk. Shein atoa wiki moja kukomeshwa hila Bandarini.

JITIHADA za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuziimarisha huduma za bandari haziwezi kufanikiwa iwapo waliopewa dhamana za kuzisimamia na kufanya kazi bandarini hapo wataendelea kufanya kazi kwa mazoea.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo katika hafla ya uzinduzi wa vifaa vipya vya kufanyia kazi bandarini, hafla iliyofanyika katika Bandari ya Malindi mjini Unguja ikiwa ni miongoni mwa shamrashamra za miaka 53 ya Mapinduzi ya matukufu ya Zanzibar.

Aliwataka wafanyakazi Bandarini hapo kuwa waaminifu na waadilifu zaidi, kuepuka urasimu katika kutoa huduma, kujiepusha na vitendo vya rushwa na zaidi kuhakikisha kuwa wateja wanahudumiwa kwa muda mchache bila ya kukiuka taratibu ziliopo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alikemea tabia ya baadhi ya wafanyakazi wa Bandari kufanya kazi kinyume na maadili na taratibu za kazi zao na kueleza kuwa endapo wakijulikana wale wote wanaofanya kazi hivyo watashughulikiwa ikiwa ni pamoja na kushtakiwa ama kufukuzwa kabisa kazi.

Pia, Dk. Shein alieleza jinsi ya mapato yanavyopotea katika Bandari hiyo ya Zanzibar kutokana na wafanyakazi wachache wasiotimiza wajibu wao ipasavyo ambao hufanya hila na udanganyifu ikiwa ni pamoja na kupitisha  vitu vilivyopitwa na muda wa matumizi vikiwemo vyakula.

Kutokana na hilo, Dk. Shein ametoa wiki moja mambo hayo yasitokee tena, ikiwa ni pamoja na kukomesha hila zinazofanywa bandarini hapo na baadhi ya wahusika za kutoa makontena bure na kupelekea kuikosesha Serikali mapato.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa hatua ya ununuzi wa vifaa hivyo ni mafanikio ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa CCM ya mwaka 2015 hadi 2020 ambayo imeanza kutekelezwa kwa kasi ikiwa ni pamoja na kuiendeleza Bandari ya Malindi kwa kuipatia vifaa na kukamilisha ujenzi wa bandari mpya ya kuhudumia mizigo katika eneo la Mpigaduri.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa Serikali itaiimarisha na kuiendeleza Bandari ya Mkoani kwa kuipatia vifaa vya kisasa vya kuhudumia abiria na mizigo ambapo pia, Serikali inaendeleza mazungumzo na wawekezaji kwa lengo la kuiimarisha Bandari ya Wete kutokana na umuhimu wake kwa Serikali, wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba na watumiaji wote.

Kwa upande wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Dk. Shein alisema kuwa Serikali itaendelea kuiimarisha gati ya Mkokotoni kwa kukamilisha ujenzi wa jeti kwa ajili ya huduma za usafiri wa wananchi hasa wa Mkokotoni na Tumbatu.

Dk. Shein alisisitiza haja kwa uongozi wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji pamoja na Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika hilo kuwaangalia wafanyakazi wanaoendesha vifaa hivyo kiafya na kimaslahi na kutoa pongezi zake kwa ununuzi wa vifaa hivyo.

Nae  Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Usafiorishajim Ali Abeid Karume alisema kuwa mafanikio hayo yametokana na uongozi bora wa Dk. Shein ambapo licha ya azma ya Serikali kujenga Bandari mpya huko Mpigaduri lakini alisisitiza haja ya kununuliwa vifaa hivyo muhimu bandarini hapo.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mustafa Aboud Jumbe alisema kuwa jumla ya TZS Bilioni 11.8 zimetumika katika kununua vifaa hivyo vikiwemo Kreni 2, Terminal Tractor 2, Terminal Trailer 2, Reach Stacker 3, Empty Container Hanler 1, Forklift 3 na maboya ya solar 7.

Alisema kuwa vifaa hivyo vinatoka nchini Sweden, Belgium, Italy na Ujerumani ambapo vimeingia nchini kati ya Mei hadi Disemba, 2016 na tayari vimeanza kutumika kwa majaribio ambapo alisisitiza kuwa kuwasili kwa vifaa hivyo kutasaidia sana kuongeza uwezo wa Bandari kuhudumia mizigo pamoja na kuongeza kasi ya ushushaji na upakiaji wa mizigo.

Viongozi mbali mbali walihudhuria katika hafla hiyo akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid na viongozi wengine wa Serikali vyama vya siasa na dini.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk.
chanzo: zanzibar24.

Comments