Uchaguzi Dimani: CUF mtegoni.

cuf benderaTUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kupitia kwa Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume hiyo, Ramadhan Kailima imesema mikutano ya kisiasa itaruhusiwa wakati wa kampeni za uchaguzi katika Jimbo la Dimani Zanzibar na kata 22 ambazo zitafanya uchaguzi wa madiwani na mikutano hiyo inatakiwa kufanyika katika maeneo husika tu, huku ikieleza kuwa kwa mgombea wa CUF atatakiwa kusainiwa fomu zake na viongozi wote wa juu wanaotambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa.
“Fomu rasmi ni kuanzia Desemba 15 hadi 22 ambapo huchukua siku saba na kampeni zitaanza Desemba 23 hadi Januari 21, mwakani. Kumekuwa na maswali mengi juu ya agizo la serikali kupiga marufuku mikutano ya vyama vya siasa lakini mikutano hiyo itaruhusiwa kwenye maeneo yatakayofanya uchaguzi,” alifafanua Kailima.
Kuhusu Chama cha Wananchi, alisema Kipengele cha 4(5) (iii) kinasema fomu za wagombea kwenye chama chenye mgogoro zisainiwe na viongozi wakuu wote wawili kwa vile wamethibitishwa na Msajili wa Vyama vya Siasa.
Alisema kama CUF ina mgogoro mgombea atakayependekezwa atatakiwa kupitisha fomu zake na kusainiwa na viongozi wote wawili wea chama hicho kutokana na kutambulika na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa.
Uchaguzi wa ubunge katika Jimbo la Dimani, Zanzibar unafanyika kutokana na kifo cha Mbunge wa jimbo hilo, Hafidh Ali Tahir aliyefariki alfajiri ya kuamkia Novemba 11, mwaka huu kwenye Hospitali ya Mkoa wa Dodoma.
 chanzo;zanzibar24.

Comments