Balozi Seif asaini kitabu cha maombolezo cha Fidel Castro.

2014Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ametia saini Kitabu cha Maombolezo kufuatia kifo cha Rais Mstaafu wa Jamuhuri ya Watu wa Cuba Marehemu Fidel Alejandro Castro Ruz  kilichotokea Tarehe 25 Novemba 2016 katika Mji wa Biran Nchini Cuba.

Utiaji saini huo wa Kitabu cha Maombolezo ameufanya katika Makaazi ya Balozi wa Jamuhuri ya Watu wa Cuba Nchini Tanzania uliopo Bara bara ya Ali Bin Said Mtaa wa Namanga Jijini Dar es salaam.

Balozi Seif  ameiwakilisha Serikali ya Mainduzi ya Zanzibar katika utiaji saini huo akiambatana na Naibu Waziri wa Afya Zanzibar  Mh. Harus Said Suleiman , Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mihayo Juma Nhunga pamoja na Mratibu Mkuu wa Ofisi ya Uratibu wa shughuli za SMZ  Dar es salaam Nd. Issa Mlingoti Ali.

Akimfariji Balozi wa Jamuhuri ya Watu wa Cuba Bwana  Jorge  Luis Loez baada ya saini hiyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Kifo cha Jemedari huyo wa Taifa la Cuba hakikuacha pengo kwa nchi hiyo lakini pia kimeigusa Tanzania kutokana na Mataifa hayo kufanana katika harakati zao za kupigania Uhuru kutoka makucha ya Kikoloni.

Balozi Seif alisema Jamuhuri ya Cuba ni kaka wa Tanzania katika njia ya kusaidia maendeleo na nyanja za uchumi zilizopata ufanisi mkubwa kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na Wataalamu wa Nchi hiyo kuwawezesha Kitaaluma wananchi Wazalendo wa Tanzania.

Akitoa shukrani zake  Balozi wa Jamuhuri ya Watu wa Cuba Nchini Tanzania Bwana Jorge Luis Lopez alisema Cuba itaendele kuwa mshirika mkubwa wa Tanzania katika azma yake ya kuona wananchi waliowengi wa ngazi ya chini wa Mataifa hayo wanafaidika na Uhuru walioupata kutoka katika makucha ya wakoloni.

Balozi Lopez alisema Cuba na Tanzania zimeshirikiana kwa muda mrefu uliobakia kuwa Historia kwa sasa hasa katika sekta za Afya, Kilimo, Viwanda na masomo ya Elimu ya Juu, ushirikiano uliowekwa msingi wake  na Waasisi wa Nchi hizo Mbili Marehemu Mwalimu Julius K. Nyerere na Bwana Fidel Castro.

Marehemu Fidel Castro alizaliwa Mnamo Tarehe 13 Agosti mwaka 1926 ndani ya familia ya watoto Sita akiwa watatu  wa Mzee Angel aliyekuwa mfanyakazi wa mashamba ya miwa akiwa na asili ya Taifa la Hispania.

chanzo; zanzibar24.

Comments