Wizara ya Afya: Kuna ongezeko kubwa la watoto wanaougua kisukari.

Waziri wa Afya Zanzibar Mahmoud Thabit Kombo akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake Mnazi mmoja katika kilele cha maadhimisho ya siku ya kisukari duniania. Picha na Makame Mshenga/Maelezo Zanzibar.Wizara ya afya Zanzibar imesema imeshtushwa na ongezeko kubwa la watoto wachanga wanaougua ugonjwa wa kisukari kunakosababisha kutumia fedha nyingi za kuwapatia matibabu.

Akizungumza na wandishi wa habari katika kuadhimisha siku ya ugonjwa wa kisukari duniani waziri wa wizara hiyo Mh. Mahamoud Thabit Kombo amesema ugonjwa huo umegunduliwa zaidi kwa watoto kutoka familia masikini.

Amesema utafiti uliofanywa na wizara hiyo kuanzia mwaka 2010 hadi 2015 umegundua zaidi ya watoto mia mbili na ishirini (220) wenye umri chini ya miaka mitano wanaugua ugonjwa wa kisukari kati yao 20 wamefariki dunia.

Aidha wizara hiyo pia imegundua zaidi ya wafanyakazi wa serikali 190 kati ya 600 waliochunguzwa afya zao hivi karibuni wamo katika hatari ya kukumbwa na ugonjwa wa kisukari.

Waziri Kombo amesema takwimu hizo zinaonesha bado wananchi wanapuza taaluma inayotolewa na watalaamu wa afya ya kujikinga na ugonjwa huo kwa kutumia vyakula vya mafuta, kushindwa kufanya mazowezi na kupima afya zao.

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa Zanzibar mwaka 2011 umegundua zaidi ya watu elfu 50 wanaugua ugonjwa wa kisukari wenye umri kati ya miaka 25 hadi 64.

Siku ya kisukari duniani huadhimishwa kila ifikapo Novemba 14 ya kila mwaka na kwa hapa Zanzibar siku hiyo imeadhimishwa kwa makongamano na mchezo wa mpira wa miguu.

chanzo;Zanzibar24

Comments