Uchaguzi mkuu bado watafuna uhusiano wa Ukawa, CUF.

Mwenyekiti wa Taifa wa CUF, Profesa Ibrahim LipumbaWANACHAMA na viongozi wa Chama cha Wananchi (CUF) wa wilaya za Mkoa wa Morogoro wamemwomba Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba kutoa azimio la kujiengua ndani ya ushirikiano wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).

Hatua hiyo ya wanachama na viongozi hao imetokana na wao kubainika ukiukwaji wa malengo ya kuasisiwa kwa umoja huo na badala yake ulitumiwa na vyama shirikishi kukihujumu ambapo kuanzia uchaguzi wa Serikali za Mitaa na ule Mkuu uliofanyika Oktoba 25, mwaka 2015.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mkutano wa ndani wa chama hicho uliowashirikisha baadhi ya wanachama na viongozi wa kamati za utendaji za wilaya za Kilosa, Mvomero, Morogoro Mjini na Vijijini kichama, walimtaka Profesa Lipumba kuiondoa CUF ndani ya Ukawa kutokana na madhara makubwa waliyoyapata.

Katibu wa Wazee wa CUF Wilaya ya Morogoro Mjini, Mohammed Chunga alisema kutokana na kutokuwepo makubaliano ya kisheria ya kuachiana majimbo na kata kutoka miongoni mwa washirika, kumekiathiri chama kutokana na maeneo yaliyoachiwa CUF kuwekewa pia wagombea wa Chadema, hatua hiyo ni pamoja na ngazi za udiwani.

Hivyo alisema sehemu ambapo mgombea wa CUF alikuwa akikubalika, pia Chadema iliweka mgombea wake na kusababisha kura kugawanyika kitendo kilichokinufaisha Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa mgombea wao kushinda kwa tofauti chache za kura.

“Ukawa ndiyo chanzo kilichotuumiza sisi CUF bila kujitambua, hata pale tulipokuwa tunakubalika na kuachiwa nafasi ya kusimamisha mgombea ili tuungwe mkono na wenzetu washirika Chadema, NCCR Mageuzi pamoja na NLD...tulijikuta tunawekewa mgombea wa Chadema...hili limetuumiza,” alisema Chunga.

Na baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya CUF Wilaya ya Morogoro Mjini, Pilly Bilali, Awadhi Komba na Katibu mstaafu wa wilaya hiyo, Haruna Msuku, kwa nyakati tofauti walisema hakuna mwanaCUF asiyetambua Ukawa umewadhoofisha kisiasa upande wa Tanzania Bara na kikinufaisha Chadema, hivyo kutaka ijiondoe mara moja.

Hata hivyo, wanachama na viongozi hao walimpongeza Profesa Lipumba kwa uamuzi wake kurudi kwenye wadhifa wake na kwamba wataendelea kumuunga mkono ili arudishe hadhi ya chama hicho baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu mwaka jana.

Akijibu hoja za wanachama na viongozi wa CUF wa wilaya hizo, Profesa Lipumba alisema ushirikiano ndani ya Ukawa, vyama washirika viliwahujumu katika uchaguzi uliopita. Profesa Lipumba alisema vyama washirika walitumia mbinu mbalimbali ili kuwadhoofisha kwenye majimbo na kata tofauti na makubaliano ya awali.

Hivyo alisema kutokana na wanachama na viongozi wa CUF sehemu mbalimbali alizopita kukutana nao moja ya tatizo kubwa waliloliona ni changamoto walizokutana nazo wagombea kwenye majimbo ya uchaguzi ulipita na kwamba chama hakiwezi kurudia makosa hayo katika uchaguzi ujao.

Alisema Ukawa ilianzishwa na vyama vinne CUF, Chadema, NCCR-Mageuzi na NLD kwa lengo la kusimamia Rasimu ya Katiba ya Jaji mstaafu Joseph Warioba na ili kuitetea, walianzisha Umoja wa Katiba ya Wananchi, hivyo kuondoa tofauti zao za kivyama kwa msingi wa utetezi wa rasimu hiyo.

Hivyo alisema Ukawa si chama cha siasa na umekuwa kwa upande wa Tanzania Bara na hautambuliki kwa mujibu wa sheria ya uanzishwaji wa vyama vingi kwa maana hiyo kazi yake ni utetezi pekee wa rasimu ya Katiba ya Jaji mstaafu Warioba na kwamba uhalali wake kwa sasa hauna nguvu.

Alisema ushirikiano ndani ya vyama vya siasa upo kwa njia nyingi na na iwapo utahitajika ni vyema ukajulikana kwa mujibu wa makubaliano ya kisheria na si ilivyo sasa. Mbali na yaliyojitokeza siku za hivi karibuni ndani ya CUF, Profesa Lipumba alitumia fursa hiyo kumtaka kila mwanachama kushikamana na kuweka tofauti zao pembeni ili kukijenga upya chama hicho.

chanzo;habarileo.

Comments