Sakaya: Kuzuiliwa ziara za Maalim wasilaumiwe polisi.

sakayaNaibu Katibu Mkuu wa CUF Bara (anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili) Bi. Magdalena Sakaya amesema Maalim Seif hakufuata katiba ya CUF na kwamba ndiyo sababu ya kuzuiliwa kufanya ziara mkoani Lindi na Mtwara, kutokana kwamba waliyo ratibu ziara zake hawakuwa na mamlaka kikatiba.

“Katibu wa chama wilaya huandika barua ya kuomba kibali cha kufanya ziara na kuipeleka polisi, kilichotokea alimtumia katibu wa Jumuiya ya Vijana CUF ambaye katiba haimruhusu na kwamba makatibu wa wilaya husika wenye mamlaka walitoa taarifa polisi ya kutoitambua ziara yake,” amesema na kuongeza.

“Polisi walipoona kuna mgongano wakazuia ziara kwa kuhofia fujo walichokifanya ni kusitisha ili wakubaliane, jambo ambalo hawakulifanya.”

Sakaya amedai kuwa”Katiba ya CUF ibara ya 96 kipengele cha 1 ukurasa wa 87 inaeleza kuwa Naibu Katibu Mkuu ana mamlaka ya kuratibu ziara za viongozi, sambamba na makatibu wa chama ngazi za wilaya ndio wenye mamlaka ya kuratibu ziara za viongozi na ndio maana uongozi wa serikali na vyombo vya dola hufanya maamuzi kwa kutumia katiba yetu,”

Amesema kilichotokea kwa Maalim Seif katika mikoa ya kusini, kitaendelea kutokea katika wilaya yoyote Tanzania Bara.

Novemba 19, Jeshi la polisi mkoani Mtwara lilizuia Mkutano wa ndani wa Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad uliotarajiwa kufanyika mkoani humo.

chanzo;zanzibar24. 

Comments