Serikali yatenga bilioni 70/- za dawa.

SERIKALI imesema imetenga Sh bilioni 70 kwa ajili ya kukabili ukosefu wa dawa nchini, huku ikitangaza kujenga kiwanda cha dawa mkoani Simiyu.

Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan alisema hayo jana wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa Sekta ya Afya, wakiwamo waganga wa mikoa na wilaya.

Awali akimkaribisha Makamu wa Rais, Mwenyekiti wa Waganga hao, Dk Sudi Leonard katika risala, alisema kuna tatizo la ukosefu wa dawa na vifaa tiba katika baadhi ya vituo vya afya nchini hali ambayo inazua malalamiko kwa wananchi.

“Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na mambo yote lakini tuna changamoto ya ukosefu wa dawa na vifaa tiba hali hii imekuwa ikisababisha malalamiko kwa wananchi. Mchakato wa upatikanaji wa dawa pia umekuwa ukichukua muda mrefu kutoka MSD mpaka kufika sehemu husika pia kuna hili kundi la watu maalumu na wao wanapokosa hulalamika,” alisema Dk Leonard.

Akifafanua kuhusu juhudi za serikali kumaliza tatizo hilo, Makamu wa Rais alisema fedha hizo zitanunua dawa, ambazo zitaenda moja kwa moja katika vituo vya afya. Samia alisema, “tumetenga Shilingi bilioni 70 kwa ajili ya kumaliza tatizo la dawa nchini pia tumetenga jumla ya Shilingi bilioni 85 kwa ajili ya kupunguza deni MSD nia yetu ni kutaka huduma za afya ziwe zenye ubora.”

Pamoja na utoaji wa fedha kwa ajili ya kuondoa tatizo hilo, Makamu wa Rais alisema mpango wa muda mrefu wa serikali ni kuwa na kiwanda cha dawa na kwamba mpango upo wa kujenga kiwanda hicho katika mkoa wa Simiyu.

“Tuna maombi ya viwanda kama nane au tisa vya dawa na sasa tunahangaika kufungua kiwanda kikubwa cha dawa katika mkoa wa Simiyu lengo likiwa ni kukabiliana na tatizo la dawa pamoja na ile azma yetu ya Tanzania ya Viwanda,” alisema.

Vilevile aliitaka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, kuhakikisha waganga wa tiba asili wote wanasajiliwa kutokana na umuhimu wao katika jamii. “

Tiba mbadala na tiba asili ni taaluma yenye asili ya Kiafrika tuliyorithi kutoka kwa mababu zetu kutokana na uhitaji wake mkubwa ninaagiza wizara kuhakikisha waganga wa tiba asili wote wanasajiliwa na wanafahamika,” alisema. 

Aliwataka wataalamu hao wa afya, kutosita kuwachukulia hatua kali za kinidhamu wote wanaobainika kukiuka maadili na viapo vyao vya kazi.

chanzo;habarileo.

Comments