WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Issa Haji Gavu, amesema Sera ya Diaspora ipo katika hatua ya mwisho
kupelekwa katika Baraza la Wawakilishi.
Gavu amesema hayo wakati alipozungumza na gazeti hili akielezea
juhudi zinazochukuliwa na Ofisi ya Rais kuhusu Sera ya Wazanzibari
wanaoishi nje ya nchi (Diaspora) ambayo imechukua muda mrefu huku jamii
hiyo ikisisitiza kutayarishwa ili iweze kutoa mchango wake katika taifa.
Amesema sera hiyo ambayo imechukua takribani miaka mitatu kujadiliwa
na kupitiwa pamoja na serikali kupokea maoni tofauti kutoka kwa wadau na
sasa imepitishwa na kujadiliwa katika ngazi ya makatibu wakuu.
“Sera ya Diaspora tayari ipo katika hatua nzuri imepitishwa na
makatibu wakuu na sasa inatarajiwa kwenda katika ngazi ya Baraza la
Mapinduzi kwa hatua za mwisho kabla ya kufikishwa mbele ya Baraza la
Wawakilishi,” amesema Gavu.
Amesema Sera hiyo ni muhimu kwa sababu ndiyo muongozo ambao
utawawezesha Watanzania wanaoishi nje ya nchi kuchangia maendeleo ya
taifa kikamilifu katika sekta mbalimbali pamoja na jamii hiyo
kutambuliwa na serikali.
Gavu alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejizatiti kuona
kwamba sera hiyo inakamilika na kuwasilishwa mbele ya Baraza la
Wawakilishi kwa ajili ya utekelezaji wake na ndio maana hivi karibuni
Zanzibar ilikuwa mwenyeji wa mkutano wa tatu wa Diaspora kitaifa.
Hivi karibuni katika Mkutano wa Kimataifa wa Diaspora uliofanyika
Zanzibar, Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein alizitaka taasisi
zinazohusika na masuala ya Diaspora, kuharakisha kukamilisha sera hiyo
ili wahusika wachangie maendeleo ya taifa.
chanzo;habarileo.
Comments