Wasimamishwa kazi kwa kituo kutokamilika.

MAMENEJA wawili wanaosimamia Kituo cha Kupozea Umeme cha Kurasini, Dar es Salaam wamesimamishwa kazi kutokana na kutokamilisha ujenzi wa kituo hicho.

Aidha, Meneja Miradi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Emmanuel Manirabona ametakiwa kutoa maelezo ni kwa nini kituo hicho hakijakamilika tangu kilipoanza kujengwa mwaka 2012 na kutakiwa kukamilika Novemba, 2013.

Hayo yalibainishwa jana Dar es Salaam na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk Medard Kalemani wakati alipotembelea vituo vya kupozea umeme vya Kurasini, Mbagala na Gongo la Mboto ambavyo ujenzi wake haujakamilika.

Dk Kalemani alisema kutokukamilika kwa vituo hivyo ndio kunasababisha kuendelea kwa tatizo la umeme jijini Dar es Salaam hivyo aliagiza ifikapo Septemba mwaka huu, jiji hilo liwe linapata umeme wa uhakika kutoka katika vituo vyake vitatu ili kuondoa tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara.

Alisema katika vituo hivyo, kazi zimeonekana kusuasua kutokana na watendaji wa Tanesco kukaa ofisini pekee bila kufuatilia maendeleo ya mradi huo.

Alisema Tanesco wanatakiwa kukamilisha ujenzi wa vituo hivyo pamoja na kuunganisha umeme kutoka Gongo la Mboto hadi Mbagala ifikapo Septemba mwaka huu ili kuwa na umeme wa kutosha.

“Miradi hii ilianza mwaka 2012 na ilitakiwa kuchukua miezi 18 pekee, yaani hadi 2013 iwe imekamilika. Lakini mpaka sasa kituo cha Kurasini hakuna kinachoendelea na meneja wake hayupo kazini. Mameneja wa kituo hiki cha Kurasini wasimamishwe…nikija Jumanne nikute meneja wengine na wewe ambaye ni Meneja Miradi hadi ifikapo Jumanne (wiki ijayo) uwe umeandika barua ya kujieleza ni kwa nini mradi umecheleweshwa. Pia tutachunguza kiasi cha fedha kilichotumika kwenye mradi na kazi iliyofanywa.”

Meneja wa Miradi, Manirabona alisema Kituo cha Kurasini kilitakiwa kianze kujengwa mwaka 2012 na kukamilika Novemba 2013, lakini mpaka sasa wanasubiri vifaa.

Alisema mkandarasi alipewa malipo yake kwa asilimia 80 na kwamba kazi aliyoifanya ni sawa na asilimia 50, lakini tangu Machi mwaka jana mkandarasi hayupo kituoni hapo.

Alieleza kuwa katika Kituo cha Mbagala walitarajia kuanza kupokea umeme kutoka Gongo la Mboto, Desemba mwaka huu na kwamba kesi iliyokuwa mahakamani ndio iliweka zuio la kuendelea kwa kituo hicho, lakini kesi ilimalizika Mei mwaka huu.

chanzo;habarileo.

Comments