MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan, amewataka wakadiriaji majenzi
nchini wahakikishe wanafanya kazi kwa kuzingatia maadili na waepuke
vitendo vya rushwa katika mchakato wa ukadiriaji majengo nchini.
Alitoa agizo hilo jana wakati akifungua mkutano wa mwaka wa
wakadiriaji majenzi kutoka nchini mbalimbali za Afrika jijini Dar es
Salaam.
Alisisitiza kuwa kwa sasa serikali ipo kwenye mchakato wa kuanza
kutekeleza miradi mikubwa ya kiuchumi ikiwemo ujenzi wa reli ya kati kwa
kiwango cha kisasa na ujenzi wa bomba la mafuta kutoka nchini Uganda
hadi Tanga.
Pia, alitaja suala la kuhamishia Makao Makuu Dodoma na kusema kuwa ni
muhimu kwa wakadiriaji majenzi kujipanga vizuri kutekeleza miradi hiyo
kwa kuweka gharama nafuu kulingana na hali halisi ya mradi unaotakiwa
kujengwa.
Alisema serikali inatambua mchango wa wataalamu wa ukadiriaji majenzi
hivyo ni muhimu wakaongeza bidii katika utekelezaji wa kazi zao hasa
kwa kuzingatia teknolojia za kisasa.
Samia alihimiza ushirikiano kati wakadiriaji majenzi wa Tanzania na
wa nchi nyingine za Afrika katika kubadilishana uzoefu, ili kuongeza
ubunifu na ufanisi katika miradi wanayopata.
Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa
Makame Mbarawa alisema serikali imetenga Dola za Marekani bilioni 2.4
kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ukiwemo
ujenzi wa barabara, madaraja na bandari na viwanja wa ndege hivyo
serikali inahitaji wakadiriaji majenzi waadilifu katika utekelezaji wa
miradi hiyo.
chanzo;habarileo.
Comments