SERIKALI kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya
Ufundi, imezindua rasmi mradi mkubwa wa ukarabati na ujenzi wa vyuo vya
ualimu nchini, lengo likiwa kuwajengea wanachuo na wakufunzi mazingira
mazuri ya kufundishia na kujifunzia.
Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika katika Chuo cha Ualimu
Kitangali mkoani Mtwara mwishoni mwa wiki, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu,
Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Maimuna Tarishi alisema
gharama ya ujenzi katika vyuo vya ualimu vinne itakuwa Sh
36,475,000,000.
Alivitaja vyuo hivyo kuwa ni Kitangali iliyopo Newala, Mpuguso
iliyopo Rungwe, Ndala iliyopo Nzega na Chuo cha Ualimu Shinyanga
kilichopo Manispaa ya Shinyanga.
“Suala la kutoa elimu bora lina mambo mengi ndani yake, ili kutimiza
dhamira hii inahitajika kuwa na walimu wa kutosha, vitendea kazi,
mitaala, vitabu na uboreshaji wa miundombinu, jambo ambalo limeanza
kufanyiwa kazi katika mwaka huu wa fedha,” alisema Tarishi.
Aidha, alisema gharama za ujenzi wa miundombinu mipya katika chuo cha
Kitangali ni shilingi bilioni nane na kwamba kuanza kwa ujenzi wa chuo
hicho ni kuashiria kuanza pia kwa ukarabati na ujenzi katika vyuo
vingine vilivyopo katika mpango huu wa awamu ya kwanza, kwa lengo la
kuhakikisha mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia.
“Shilingi bilioni nane zitakazotumika katika ujenzi wa hapa Kitangali
zinapaswa kuleta manufaa kwa wananchi wanaozunguka chuo hichi, hivyo
nawaasa wakandarasi kuwatumia wananchi wa maeneo yanayozunguka chuo,”
alisisitiza Katibu Mkuu.
Akizungumzia ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kitangali, Katibu Mkuu alisema
baada ya kutembelea chuo hicho na kuiona miundombinu yake jinsi
ilivyochaa alijiridhisha kwamba haiwezi kukarabatiwa na kukubaliana
ufanyike ujenzi wa miundombinu mipya.
Naye Ofisa kutoka Idara ya Elimu ya Ualimu, Fredrick Shuma alisema
mradi wa ujenzi na ukarabati wa vyuo vya ualimu vinne unafadhiliwa na
Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Canada kupitia
Shirika la Mambo ya Nchi za Nje na Maendeleo ya Biashara ambayo
inachangia Sh bil 28. 27 na Serikali ya Tanzania inachangia kiasi cha Sh
bil 8.2.
“Ujenzi na ukarabati wa vyuo hivyo vinne ukikamilika utaongeza
udahili wa wanachuo kutoka 1,643 hadi kufikia 2,950 hivyo kuongeza
wanachuo 1,318 katika vyuo hivyo vinne,” alifafanua ofisa huyo wa Idara
ya Elimu ya Ualimu.
chanzo;habarileo.
Comments