WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka viongozi wa wilaya za Temeke
na Kigamboni iliyozaliwa kutoka ubavuni mwa Temeke, kuanza kugawana mali
badala ya watumishi.
Agizo hilo limekuja baada ya Kigamboni kupata Mkuu mpya wa Wilaya ambaye ni Hashim Mgandilwa.
Waziri Mkuu alisema hatua hiyo itasaidia kuondoa migogoro baina ya
pande hizo kwani watagawana mali wakiwa wamoja. Akizungumza na watumishi
wa Manispaa ya Temeke mkoani Dar es Salaam hivi karibuni, Majaliwa
alisema kuanza kugawa watumishi kabla ya mali kumesababisha maeneo mengi
kuwa na ugomvi usiokoma, akitolea mfano Mbinga na Nyasa, mkoani Ruvuma.
Alisema wanapogawana sasa watafanya kwa haki, lakini wakishagawa
watumishi watakuwa wanavutia kwao huku ugomvi ukihamia hadi katika
Baraza la Madiwani watakaokuwa wanatumwa na watendaji.
Alisema pia Meya wa Temeke kama kata yake itaangukia Temeke atabaki
kuwa meya wa huko lakini kama ataangukia Kigamboni, italazimu kufanyika
upya kwa uchaguzi wa meya. Pia amewahimiza watendaji Manispaa ya Temeke
kuimarisha makazi mapya kwa kuhamasisha ujenzi wa majengo ya kisasa
tofauti na mengi yaliyojengwa kiholela.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alisema katika
kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya, amezungumza na Balozi
wa Japan nchini na kukubali kujenga sehemu za kutoa huduma ya dharura
kwa haraka.
Alisema kwa kuanzia watajenga katika Manispaa ya Temeke na kufuatia
katika wilaya nyingine za Ilala na Kinondoni kutokana na takwimu
zikieleza watu nusu ya wagonjwa 6,000 wa kila siku wanahitaji huduma ya
haraka kila siku katika jiji hilo.
chanzo;habarileo
Comments