Kipilimba bosi mpya Usalama wa Taifa.

RAIS John Magufuli amemteua na kumwapisha Dk Modestus Francis Kipilimba kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS).

Dk Kipilimba aliapishwa Ikulu Dar es Salaam jana mchana, saa chache baada ya uteuzi wake uliotangazwa asubuhi.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu, baada ya kuapishwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa, Dk Kipilimba alikula kiapo cha Uadilifu kwa Viongozi wa Umma kilichoongozwa na Kamishna wa Maadili, Jaji mstaafu Salome Kaganda.

Kabla ya uteuzi huo, Dk Kipilimba alikuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), na amechukua nafasi iliyoachwa wazi na Rashid Othman ambaye amestaafu utumishi wa umma mwishoni mwa wiki iliyopita.

Aidha, Rais Magufuli alimteua Robert Msalika Makungu kuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa Tanzania Bara.

Kabla ya uteuzi huo, Makungu alikuwa Ofisa Ubalozi katika Ubalozi wa Tanzania nchini Ethiopia. Pia Rais Magufuli amemteua aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa, George Madafa kuwa Balozi na nchi atakayopangiwa itatajwa baadaye.

Taarifa ya Ikulu ilieleza kuwa wakurugenzi na naibu wakurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa waliopo wanaendelea na nafasi zao.

chanzo;habarileo.

Comments