WILAYA ya Kinondoni inatarajia kuanza kutumia mfumo mpya wa kadi za matibabu katika hospitali na zahanati za wilaya hiyo utakaozinduliwa hivi karibuni.
Hayo yalisemwa jijini hapa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Ally Hapi wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema wilaya hiyo itakuwa ni wilaya ya kwanza katika mkoa huo kuanza kutumia mfumo huo, ambao kila mkazi wa Kinondoni atatakiwa kutoa Sh 40,000 kwa mwaka na kupatiwa kadi hiyo ambayo ataitumia atakapokwenda hospitali bila kuchajiwa kiasi kingine cha fedha.
Hapi alisema mfumo uliopo kwa sasa unatumia muda mwingi na kusababisha wananchi kupoteza muda kupata huduma wakati angekuwa na kadi angeweza kupunguza muda wa foleni na kuendelea na mambo mengine.
“Kumekuwa na misururu na misongamano katika hospitali zetu lakini kwa kutumia kadi hii foleni hizo zitapungua kwa kiasi kikubwa na kuongeza ufanisi katika huduma hii ya afya katika wilaya yetu na utakuwa ni mfumo rahisi wenye gharama nafuu ambapo kila mwananchi ataweza kutumia,” alisema Hapi.
Aliongeza kuwa kuanzishwa kwa mfumo huo kutasaidia kuongeza ufanisi katika sekta ya afya pamoja na kupunguza mianya ya rushwa iliyopo katika baadhi ya vituo vya afya.
“Hizi kadi zitakuwa ni suluhisho la mambo yote hayo, ukishalipia Sh 40,000 yako kwa mwaka ambayo kwa mwezi itakuwa ni Sh 3,300 hutatakiwa kulipa chochote wakati wote wa matibabu,” alisisitiza.
chanzo;habarileo.
Comments