UN yatoa ripoti ya matukio ya vitendo viovu vya kingono vya askari wa Kofia Buluu.

Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa tangu ulipoanza mwaka huu wa 2016 yameripotiwa matukio 44 ya vitendo viovu vya kingono vilivyohusisha askari wa kulinda amani wa Kofia Buluu wa umoja huo.
Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na umoja huo, tangu ulipoanza mwaka huu wa 2016 yamegunduliwa matukio 44 ya ufisadi wa kiakhlaqi uliofanywa na askari wa kulinda amani, ambapo 29 kati ya hayo yameyawahusisha askari waliotumwa Jamhuri ya Afrika ya Kati chini ya mwamvuli wa kikosi cha kulinda amani nchini humo MINUSCA.
Ripoti hiyo imeongeza kuwa matukio saba ya vitendo hivyo viovu vya kingono yamehusisha askari wa Kofia Buluu walioko nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, matukio mawili ya askari walioko nchini Haiti na mengine ya wale wanaohudumu katika nchi za Ivory Coast, Sudan Kusini na zaidi nchini Mali.
Nyaraka zinazohusiana na matukio hayo zinaonesha kuwa aghalabu ya watuhumiwa wa ufisadi huo wa kiakhlaqi ni askari wenye uraia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Jamhuri ya Kongo, Niger, Morocco na Afrika Kusini.
Hata hivyo msemaji wa Umoja wa Mataifa Stéphane Dujarric, amesema uchunguzi kuhusiana na kadhia hiyo bado haujakamilika.
Katika mwaka 2015, Umoja wa Mataifa uliorodhesha matukio 69 ya vitendo viovu vya kingono vilivyofanywa na askari wake wa Kofia Buluu wanaohudumu katika nchi mbalimbali.../
chanzo;parstoday.

Comments