Balozi Iddi: Serikali Umoja wa Kitaifa Z'bar ipo palepale.



Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, amesema anaamini kuwa, Rais Dk. Ali Mohamed Shein, atatumia hekima na busara kuchagua viongozi wa vyama vingine vya upinzani kuendeleza Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), baada ya Chama cha Wananchi (CUF) kususia uchaguzi mkuu wa marudio uliofanyika Machi 20, mwaka huu.
 
Akizungumza na Nipashe nje ya Baraza la Wawakilishi, Chukwani, mjini Zanzibar jana, Balozi Iddi alisema wa Katiba, Rais wa Zanzibar ana nafasi 10 za kuteua wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na ana amini kuwa Dk. Shein atatumia hekima na busara kuchagua viongozi wa vyama vya upinzani kuingia katika Baraza la Wawakilishi ili kuendeleza Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
 
“Sisemi kuwa wote tutakuwa wajumbe kutoka Chama cha Mapinduzi, bila shaka Rais anaweza kutumia hekima kuiendeleza Serikali ya Umoja wa Kitaifa, labda akatoa nafasi ya kiti kimoja au viwili akawapa wajumbe kutoka vyama vingine vya upinzani ili tuwe na Baraza la Wawakilishi la kweli linaloonyesha umoja wa kitaifa,” alisema Balozi Iddi ambaye juzi aliteuliwa kwa mara ya pili kushika wadhifa huo.
 
Serikali ya Umoja wa Kitaifa ilifikiwa baada ya maridhiano kati ya CCM na CUF 2009 na kumaliza kile kilichokuwa kikiitwa mpasuko wa kisiasa visiwani humo na baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 uliomuweka madarakani Dk. Shein, akisaidiwa na Makamu wake wa Kwanza, Maalim Seif Sharif Hamad (CUF) na Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Iddi na kuunda Baraza la Mawaziri lililojumuisha wabunge wa CUF.
 
Hata hivyo, vyama vilivyoshiriki uchaguzi wa marudio vimeshindwa kukamilisha sharti la kikatiba la kuunda SUK, baada ya kushindwa kufikia asilimia 10 ya kura za urais au uwakilishi.
 
Kuhusu kuteuliwa kwake, Balozi Iddi alisema anamshukuru Dk. Shein kwa kumuamini na kuahidi kuwa hatamuangusha katika utekelezaji wa majukumu yake, ikiwamo kuisimamia serikali katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
 
“Nitafanya kazi hiyo kwa uadilifu na uaminifu mkubwa, lengo letu ni kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na kuondoa kero zote zinazowakabili wananchi bila ya kujali itikadi zao, rangi, ukabila au dini zao,” alisema.
 
 Balozi Iddi alisema atahakikisha ana mshauri Rais kuunda serikali yenye kuwajibika kwa wananchi, ikiwa na watu wenye sifa na uwezo na watakaosimamia uwajibikaji pamoja na kuondoa kero za wananchi kwa haraka na kuleta mabadiliko ya Zanzibar katika nyanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa.
 
“Tunataka kufuta kero za wananchi, tukianzia na changamoto za kupatikana huduma bora za maji, afya, elimu na ajira, hii itakuwa ni serikali ya wananchi itakayozingatia changamoto zote zinazowakabili,” aliongeza kusema Balozi Iddi.
 chanzo;ippmedia.

Comments