Harusi aonya watoto wasiopata chanjo.

NAIBU Waziri wa Afya, Harusi Said Suleiman, amesema, pamoja na mafanikio ya kuwapatia chanjo watoto, bado zipo changamoto za baadhi yao kutopata chanjo au kukamilisha ratiba zao za chanjo.
Hayo aliyaeleza alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuelekea wiki ya chanjo Afrika inayotarajiwa kuanza leo ambapo kitaifa itazinduliwa Fujoni wilaya ya Kaskazini Unguja.
Alisema, watoto hao wako kwenye hatari ya kupata maambukizi ya magonjwa na kuhatarisha jamii nzima.
Alisema, lengo kuu la wiki ya chanjo ni kuhamasisha kusisitiza umuhimu wa chanjo katika kuokoa  maisha juu ya magonjwa yanayozuilika  kwa chanjo.
Alisema, kupitia wiki hii Wizara ya Afya kupitia mradi shirikishi Afya ya Uzazi na Mtoto, Kitengo cha Chanjo kitawapatia chanjo watoto wote chini ya miaka mitano na wasichana wenye umri wa miaka 14 ambao hawajapata au kukamilisha ratiba zao za chanjo.
“Chanjo ni mkakati muafaka na wa gharama nafuu katika kutokomeza maradhi na kupunguza vifo vya watoto,” alisema.
Alisema, Shirika la Afya la Kimataifa (WHO), limethibitisha kuwa chanjo huzuia takribani vifo milioni mbili hadi tatu kila mwaka kutokana na maradhi yanayokingwa kwa chanjo duniani.
Alisema hapa Zanzibar, mafanikio ya chanjo yameonekana dhahiri ikiwemo kutokomeza ugonjwa wa ndui, dondakoo, kifaduro,pepopunda ya watoto wachanga na surua.
Aidha, alisema, Zanzibar imekuwa miongoni mwa nchi zisizo na virusi pori vya polia vinavyosababisha ulemavu kwa watoto wadogo tokea mwaka 2015 na kuthibitishwa na mashirika ya kimataifa.
Alisema, mafanikio hayo yametokana kufanikiwa kuwapatia chanjo watoto walio chini ya umri wa miaka miwili nchi nzima kwa zaidi ya asilimia 85.
Hivyo, alisema, ni muhimu kuhakikiha kila mtoto anapata chanjo zake zote na kwa wakati hasa ikizingatiwa kumekuwepo na miripuko ya ungonjwa wa polio katika nchi jirani na Tanzania.
“Fursa ya wiki ya chanjo itatumika kuhamasika na kuielimisha jamii na familia kuhusu umuhimu wa chanjo, pamoja na kuwapeleka kwenye vituo vya kutolea huduma hiyo ili wakapate chanjo,” alisema.
Naibu Waziri, aliyataja magonjwa yanayokingwa kwa chanjo hapa nchini kwa saa ni kifua kikuu,dondakoo,kifaduro, polio, surua rubella na pepopunda.
Magonjwa mengine ni homa ya ini, homa ya uti wa mgongo, kichoni, kuharisha na saratani ya mlango wa kizazi.
“Walengwa ni watoto wote walio na umri wa chini ya miaka miwili na wasichana wenye umri wa miaka 14 ambao hawajapata au hawajakamilisha chanjo,” alisema.
Naye Ofisa wa Kitengo cha Chanjo, Abdulhamid Ameir, alisema, wanalenga kutoa chanjo kwa watoto 56,000 kwa mwaka 2019.
Alisema, mwaka 2018 walilenga kutoa chanjo kwa watoto 54,000, lakini, waliopatiwa walikuwa 52,815 huku 4% ya watoto hawakufikiwa na huduma hiyo.
Mratibu wa Chanjo, Yussuf Haji Makame, aliwataka wananchi wenye watoto wa umri huo kuwapeleka watoto wao vituoni na kuhakikisha wanapata chanjo hiyo na kumaliza dozi ili kuwakinga na maradhi hayo na hivyo kuliwezesha taifa kuwa na kizazi chenye afya bora.
Zanzibarleo.

Comments