NAIBU Waziri wa Afya, Harusi Said Suleiman, amesema, kuna ongezeko la maradhi ya yasiyoambukiza ikiwemo saratani, hivyo, jitihada zaidi zinahitajika kuielimisha jamii kujikinga na maradhi hayo.
Hayo aliyaeleza katika maadhimisho ya siku ya saratani duniani katika hafla iliyofanyika Kwa Binti Hamrani wilaya ya Mjini Unguja jana.
Alisema, kwa mujibu wa takwimu zilizopo hospitali ya Mnazimmoja ambazo zimejumuisha wagonjwa waliofika hapo, idadi imekuwa ikiongezeka katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2015 hadi mwaka 2017.
Alisema, mwaka 2015 waligundulika wagonjwa 271 huku mwaka 2016 ikiwa na wagonjwa 392 na mwaka 2017 wagonjwa 560.
Alisema, idadi hiyo ni kubwa na yenye kutisha huku saratani ya shingo ya kizazi, matiti na tenzi dume zikiongoza.
Alisma, kati ya wagonjwa wanaogundulika na maradhi hayo, kwa asilimia kubwa wanafika hospitalini ikiwa ugonjw upo katika hatua kubwa, hali ambayo hupelekea kuongezeka kwa gharama za matibabu.
“Lakini hata athari zitokanazo na maradhi haya zinakuwa kubwa”, alisema.
Alisema, vifo vingi vinavyotokana na maradhi hayo husababishwa na kukosa au kuwa na uelewa mdogo wa namna ya kujikinga, njia za kufuata ili kuyagundua mapema na kupata tiba sahihi.
Hata hivyo, Naibu Waziri, alisema, hadi sasa hakuna daftari maalum la kuwekea takwimu za maradhi hayo, lakini, jitihada zimeanza kuchukuliwa za kuandaa daftari hilo ambapo wafanyakazi wawili wameshapatiwa mafunzo hayo.
“Hivi karibuni wafanyakazi wengine zaidi watapatiwa taaluma hiyo na mara baada ya kumalizika mafunzo mfumo wa ukusanyaji data za saratani utaanzishwa,” alisema.
Hivyo, aliitaka jumuiya ya wagonjwa wanaoishi na saratani kuendeleza jitihada zao za kuelimisha jamii juu ya kujikinga na maradhi ya saratani na kufanya uchunguzi wa afya ili kugundua mapema na kupatiwa tiba sahihi.
Alisema, jitihada kubwa zilizochukuliwa na wizara ni kuanzisha kitengo cha maradhi yasiyoambukiza ,kusomesha wafanyakazi wa afya akiwemo daktari bingwa wa uchunguzi wa maradhi ya saratani, na daktari bingwa wawili wa tiba za saratani ambao wanaendelea kufanyakazi katika kitengo cha tiba za saratani hospitali ya Mnazimmoja.
Zanzibarleo.
Comments