Mawaziri waagiza mradi wa umeme Rusumo ukamilike kwa wakati.

Mawaziri wanaohusika na utekelezaji wa mradi wa umeme wa maji wa Rusumo (MW 80)  kutoka Tanzania, Rwanda na Burundi wamekagua kazi ya ujenzi wa mradi huo wilayani Ngara mkoa wa Kagera na kutoa maelekezo mbalimbali ikiwepo kutaka mradi huo kukamilika kwa wakati.

Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani ndiye aliyewaongoza, Waziri wa Nishati na Migodi wa Burundi, Come Manirakiza na Waziri wa Miundombinu wa Rwanda, Claver Gatete katika kukagua kazi mbalimbali zinazoendelea kufanyika ikiwemo ujenzi wa eneo itakapojengwa mitambo ya kuzalishia umeme na ujenzi nyumba za wafanyakazi.

Kwa ujibu wa Dkt. Kalemani, ujenzi wa mradi huo ulianza Februari 2017 na inapaswa kukamilika ndani ya miezi 36.

“Pia tumeiagiza Bodi na wataalamu walioko katika mradi huu, wahakikishe kuwa wanashirikisha Mamlaka na Taasisi mbalimbali zilizopo katika maeneo ya mradi katika nchi zote tatu hasa katika masuala yanayohusu jamii zinazozunguka mradi na stahili za wafanyakazi ili kutokuwa na vikwazo katika utekelezaji,” alisema Dkt Kalemani.

Mradi huo unatarajiwa kuongeza Megawati 27 kwa kila nchi washirika na kujenga miundombinu ya usafirishaji umeme wa KV220 ambapo kwa Tanzania, miundombinu hiyo itajengwa kutoka Rusomo kwenye Nyakanzani ikiwa na umbali wa Kilometa 98.

Aliongeza kuwa, miundombinu hiyo ya usafirishaji umeme, kwa upande wa Tanzania, itaingiza umeme katika gridi ya Taifa kupitia njia  ya umeme inayotoka Geita na kwamba, vijiji  13 vinavyopitiwa na mradi wa Rusumo vitasambaziwa nishati hiyo.

Mradi huo unagharamiwa na nchi washirika kupitia wadau wa maendeleo ambao ni Benki ya Maendeleo Afrika (AfdB) na Benki ya Dunia (WB) ambapo kwa ujenzi wa mradi wa kuzalisha umeme kila nchi imechangia takribani Dola za Marekani milioni 113.

Comments