Waziri Rashid ataka wananchi wachangie maendeleo.

WAZIRI wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Rashid Ali Juma, amewaomba wananchi kuendelea kuchangia miradi ya maendeleo kwa manufaa ya taifa.

Akifungua mradi wa maji safi na salama katika kijiji cha Donge Mbiji ikiwa ni miongoni mwa shamra shamra za miaka 55 ya mapinduzi, alisema lengo ni kurahisisha upatikanaji wa huduma za kijamii.

Aidha alisema pamoja na kujitokeza kwa changamoto za uharibifu wa mazingira kwenye vianzio vya maji safi na salama, serikali ipo makini na inafanya juhudi kuhakikisha huduma hiyo inakuwa endelevu.

Mapema Katibu Mkuu Wizara, Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati, Alhalili Mirza, alisema  mradi huo umegharimu dola za Marekani milioni 5.5  ambapo kwa Donge zimetumika dola  za Marekani 1.8 milioni.

Alisema serikali imechangia shilingi milioni 513 kwa ajili ya malipo ya fidia na uvutaji wa umeme.

Aidha alisema mradi huo ni msaada kutoka serikali ya China na unatarajiwa kuwanufaisha watu 102,000 ambapo upande wa Donge ni watu 48,000.

Alitaja maeneo mengine yatakayonufaika na mradi huo kuwa ni pamoja na Chaani, Kisongoni, Kiboje na Miwani.

Katika hatua nyengine alisema kazi zitakazotekelezwa kupitia mradi huo ni pamoja na uchimbaji wa visima, ujenzi wa matangi,mitambo ya kutilia dawa na ulazaji wa mambomba.

Alisema utekelezaji huo unaenda sambamba malengo ya dunia (SDG), dira ya maendeleo ya taifa 2020, Mkakati wa kukuza uchumi na kupunguza umasikini Zanzibar (MKUZA III) na ilani ya uchaguzi ya CCM 2015-2020.

Nae Balozi mdogo wa China Zanzibar Xie Xiao Wn, alisema serikali ya China inashukuru kuamini na Zanzibar katika uendelezaji wa ujenzi wa miradi ya maendeleo kwa ajili ya wananchi.

Mkandarasi wa mradi huo kutoka China, Shein Qi alisifu juhudi zilizochukuliwa katika utekelezaji wa mradi huo huku akiahidi upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama endelevu.

Zanzibarleo.

Comments