Wananchi washauri wizara kuongeza ubunifu tamasha la lijalo la biashara.

WIZARA ya Biashara na Viwanda Zanzibar, imeombwa kuimarisha huduma katika maonyesho yajayo ya biashara ili kuvutia wafanyabiashara wengi zaidi pamoja na wananchi.

Wakizungumza na Zanzibar Leo, baadhi ya wananchi na wafanyabiashara waliopo katika maonyesho hayo yanayofanyika Maisara, ikiwa ni shamrashamra za miaka 55 ya mapinduzi, walisema ipo haja ya kuwekwa vifaa vya kupozea hewa (misting system) kama zinavyofanya nchi nyengine ili kupunguza joto kali liliopo eneo hilo.

Mmoja ya wananchi hao, Hamad Mohammed Haji, alisema ikiwa wizara itaweka vifaa hivyo, watavutia wananchi wengi zaidi kwa sababu eneo hilo lina joto kali.

Aidha alisema kama wizara itashindwa kuweka kifaa hicho basi inaweza kuweka ‘misting fans’ ambazo zina uwezo mkubwa wa kupoza hewa tofauti na feni za kawaida.

“Kwa kweli joto kali sana hasa kipindi hichi cha Januari ambacho maonyesho haya huwa yanafanyika, tunajua wizara yetu ni sikivu na inaweza kutuwekea mazingira mazuri sisi wafanyabiashara ili kuwapa fursa wananchi kutembelea na kupata elimu katika tasisi mbalimbali zilizopo hapa,” alisema.

Kwa upande wake, Khadija Khamis Ali, alisema joto linawakoshesha fursa wananchi kutembelea mabada hayo.

“Kwa kweli katika banda letu tulitembelewa na Rais mstaafu wa awamu ya sita, Dk. Amani Abeid Karume, lakini alishindwa kukaa kutokana na joto lililokuwepo na hata wananchi wengine wanaotembelea huwa hawakai kupata elimu kutokana na joto,” alisema.

Hivyo walitumia fursa hiyo kuiomba wizara kulifanyia kazi suala hilo ili maonyesho yajayo yawe bora zaidi.

Katika hatua nyengine, waliiomba wizara kuchanganya mfumo wa kuweka wafanyabiashara na taasisi za serikali hatua ambayo itawawezesha mwananchi kutembea na kupata elimu, badala ya mfumo wa sasa ambapo mabanda ya taasisi za serikali yamewekwa pamoja.

Comments